1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bunge la Marekani lataka msaada wa Marekani kusitishwa Yemen

Sekione Kitojo
14 Februari 2019

Baraza la wawakilishi nchini  Marekani limeidhinisha Jumatano(13.02.2019) azimio litakalofikisha mwisho uungaji mkono wa Marekani kwa muungano wa kijeshi unaoongozwa na Saudi Arabia katika vita nchini Yemen,

https://p.dw.com/p/3DMGx
US Kampfjet F/A-18C Hornet fliegt einen Angriff
Ndege za kivita za Marekani zinazotoa msaada kwa ndege za muungano unaoongozwa na Saudia katika vita vya YemenPicha: picture-alliance/dpa/MC3 Josh Petrosino

Hatua  hiyo ni  ya  imechukuliwa  wakati  wabunge  wengi  wakitaka kumlazimisha rais Donald  Trump  kuimarisha  sera  zake  kuelekea  nchi hiyo  ya  Kifalme.

Ilikuwa  mara ya  kwanza  baraza  hilo  la  wawakilishi kuunga  mkono azimio  la  madaraka  ya  vita, lakini  kura hiyo  iliyoungwa  mkono  na wabunge  248 kwa  177 waliopinga, kwa  karibu kwa  misingi ya kichama, haitatosha, hata hivyo, kuweza  kuikiuka  ahadi  ya  Trump kutoa kile  ambacho  kinaweza  kuwa  kura  yake  ya kwanza  ya  turufu.

Jemen Raketenabschuss in Aden
Vita vya YemenPicha: Getty Images/AFP/S. Al-Obeidi

Ni wabunge  18  tu  wa  chama  cha  Trump  cha Republican  katika  baraza  hilo  la  wawakilishi  waliojiunga na  Wademokrati 230 kuunga  mkono  azimio  linalotaka kuzuwia  jeshi  la  Marekani  kujiingiza  katika  uhasama ndani  ama  inayoiathiri  Yemen, ikiwa  ni  pamoja  na kutoa msaada  wa  kujaza  mafuta  katika  ndege  zinazofanya mashambulizi  katika  vita  vya  wenyewe  kwa  wenyewe nchini  Yemen, bila  ya  idhini  kutoka  katika  bunge  la Marekani  Congress.

Wademokrati  na  Warepublikani walilirejesha  tena  azimio la  madaraka  ya  kivita  wiki  mbili zilizopita kama  njia  ya kutuma  ujumbe  mzito kwa  utawala  wa  Riyadh   juu  ya maafa ya  kiutu  nchini  Yemen  na  kushutumu  mauaji  ya mwandishi  habari  wa Saudia, Jamal Khashoggi.

Türkei Istanbul Protest gegen Ermordung von Khashoggi durch Saudis
Mwandishi habari raia wa saudi Arabia aliyeuwawa Jamal KhashoggiPicha: Getty Images/AFP/Y. Akgul

Vita vimewafikisha watu katika ukingo wa  njaa

Vita  vya Yemen  vilivyodumu  kwa  zaidi  ya  miaka  minne vimewauwa  mamia  kwa  maelfu  ya  watu, kuvuruga uchumi  wa  nchi  hiyo  na  kuwafikisha  mamilioni ya  watu katika  ukingo  wa  kufa  njaa.

Utawala  huo  pamoja  na  wengi  wa  wabunge  wa  chama cha  Trump  cha  Republikani katika  baraza  la  Congress, wamesema  azimio  hilo  halistahili  kwa sababu  majeshi ya  Marekani  yamekuwa  yakitoa  msaada  wa  kutia mafuta  ndege  na  misaada  mingine  katika  mzozo  wa Yemen, na  sio  wanajeshi. Pia  utawala  huo  umesema hatua  hiyo  itaathiri  uhusiano  katika  eneo  hilo  na kuathiri  uwezo  wa  Marekani  kuzuwia  kuenea  kwa ghasia  zinazosababishwa  na  makundi  ya  itikadi  kali.

Jemen Sanaa Zerstörung
Uharibifu mkubwa unaotokana na vita nchini YemenPicha: picture-alliance/Photoshot/Hani Ali

Baraza  la  Seneti  linatarajiwa  kulipigia  kura  azimio  hilo katika  muda  wa  siku  30 zijazo.

Azimio kama  hilo  la  hapo  kabla  lilipita  katika  baraza  la Seneti kwa  kura  56 dhidi  ya  41  mwezi  Desemba. Lakini azimio  hilo  halikufikishwa  katika  baraza  la  wawakilishi , ambako  Warepublican  walikuwa  na  wingi  hadi Wademokrati  walioshika  udhibiti Januari 3  mwaka  huu, kufuatia  ushindi  mkubwa  waliopata  katika  uchaguzi  wa mwezi  Novemba.

Mwandishi:  Sekione Kitojo / rtre

Mhariri: Grace Patricia Kabogo