1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bunge la Uturuki laidhinisha mjadala wa mabadiliko ya katiba

10 Januari 2017

Bunge la Uturuki limepiga kura ya kuendeleza mjadala kuhusu marekebisho ya katiba ambayo yataongeza mamlaka ya rais Tayyip Erdogan, ikiwa ni hatua kuelekea hatua ya wadhifa wa rais kuwa na mamlaka makubwa.

https://p.dw.com/p/2VYXL
Türkei Binali Yildirim
Picha: Getty Images/E. Ortac

Erdogan na wanaomuunga mkono wanasema kuwa Uturuki inahitaji uongozi thabiti wa rais ili kuzuia kurejea kwa serikali dhaifu ya muungano, wakati huo wapinzani wake wanasema kuwa mabadiliko hayo yanachochea hatua kuelekea uongozi wa kimabavu.

Kura ya awali ambayo ni ishara ya mwanzo ya kukubaliana na muswada huo, ilipita kwa kura 338 ikionyesha kuwa baadhi ya wawakilishi wa bunge kutoka chama tawala cha AKP pamoja na chama cha upinzani MHP ambao wanakubaliana na mabadiliko hayo walipiga kura ya kuunga mkono.

Ili muswada huo uweze kupitishwa utahitaji kuungwa mkono na wawakilishi wa bunge angalau 330 kati ya viti 550 vya bunge ili iweze kupigiwa kura ya maoni. Chama cha AKP kina wawakilishi 361 wenye sifa za kupiga kura wakati MHP ina wawakilishi 39.

Mahmut Tanal, ni mbunge kutoka chama kikuu cha upinzani CHP anasema ''Mabadiliko haya sio kati ya vyama vyenye wawakilishi bungeni, bali ni kati ya wanaotaka taifa linaloongozwa na wale, na wale ni watu ambao wanapingwa na nchi ambayo inaongozwa kwa mujibu wa sheria. Mapambano haya ni kati ya wanaotaka demokrasia na wale walio kinyume na demokrasia.''

Türkei | Polizei blockiert Straße um Proteste vor dem Parlament gegen die Verfassungsänderung zu verhindern
Polisi wakiwazuia waandamanaji waliokuwa wakielekea nje ya jengo la BungePicha: Reuters/U. Bektas

Katika mabadiliko hayo Rais Erdogan atakuwa na mamlaka ya kuteua na kufukuza mawaziri katika serikali, kuchukua uongozi katika chama chake na kuruhusiwa kuwepo madarakani mpaka mwaka 2029.

Wakati wa majadiliano kuhusu muswada huo, waziri mkuu wa nchi hiyo Binali Yildirim alisema kuwa, marekebisho hayo yatasaidia kukabiliana na matatizo ambayo nchi hiyo inakabiliana nayo sasa ya kuwa na mamlaka mbili kubwa.

Kati ya wabunge 550, 480 wamepiga kura, kati ya hao 134 wamepiga kura kuukataa muswada huo. Wengine wamejizuia kuweka wazi kama wanaunga mkono au wanaupinga.

Mwandishi: Celina Mwakabwale/reuters

Mhariri: Grace Patricia Kabogo