1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bush atembelea kumbukumbu ya maangamizi ya Wayahudi

11 Januari 2008
https://p.dw.com/p/CoEp

JERUSALEM

Rais George W. Bush wa Marekani akiwa ziarani Mashariki ya Kati leo ametembelea kumbukumbu ya mangamizi ya Wayahudi mjini Jerusalem.

Yad Vashem mahala pa kumbukumbu ya maangamizi ya Wayahudi milioni sita waliouwawa wakati wa utawala wa Manazi wa Ujerumani katika Vita Vikuu vya Pili vya Dunia ni kituo ambacho kwa desturi hutembelewa na waheshimiwa wote wa kigeni wanaoitembelea Israel.

Akiwa kwenye eneo hilo la kumbukumbu Bush amesema angelitumai kwamba watu wengi watakaokwenda kulitembelea eneo hilo itakuja kuwa ni ukumbusho makini kwamba uovu upo na kwamba wakati unapokutana na uovu hakuna budi kuupiga vita.

Hapo jana Bush ametowa wito kwa Israel na Wapalestina kuchukuwa maamuzi magumu kufanikisha amani na ameitaka Israel kuacha kuikalia kwa mabavu ardhi ya Palestina ilioiteka katika vita vya mwaka 1967.Bush pia ameelezea matumaini yake kwamba makubaliano ya amani yanaweza kufikiwa mwishoni mwa mwaka huu.

Bush anatazamiwa kuondoka leo hii kuelekea Kuwait katika kituo cha pili cha ziara yake Mashariki ya Kati ambayo pia itamfikisha Bahrain,Umoja wa Falme za Kiarabu,Saudi Arabia na Misri.