1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bush hatakiwi mashariki ya kati.

8 Januari 2008
https://p.dw.com/p/CmbW

Amman.

Mahasimu wa Marekani wamemweleza moja kwa moja rais wa Marekani George W. Bush kuwa hatakiwi katika eneo la mashariki ya kati na kundi la kigaidi la al-Qaeda limewataka wafuasi wake kumpokea kwa mabomu na sio maua.

Lakini rais Bush binafsi anasema kuwa ziara yake , ambayo itamchukua hadi Israel, ukingo wa magharibi, Misr na mataifa kadha ya ghuba , ina lengo la kuimarisha hatua za kuleta amani katika mashariki ya kati zilizokwisha anza na kupata kuungwa mkono kwa juhudi za Marekani za kuidhibiti Iran.

Lakini kuna shaka miongoni mwa mataifa ya Kiarabu juu ya nafasi ya Bush kuweza kufanikisha juhudi zake za kufikiwa makubaliano ya kweli na Israel hadi atakapoondoka madarakani Januari 2009, kwa kuwa watu wengi wanaiona nchi hiyo kuwa inaipendelea mno Israel.

Waziri wa zamani wa habari nchini Jordan mshirika wa karibu wa Marekani Saleh Qallab ameisuta Marekani kwa kusema kuwa malengo ya nchi hiyo hayalingani na matarajio ya watu wa mashariki ya kati. Lakini profesa wa masuala ya siasa katika chuo kikuu cha Jerusalem amesema kuwa katika suala la Israel na Palestina, kunahitajika kila upande kuwajibika.

Viongozi wa Israel na Palestina wanatarajiwa kukutana leo Jumanne kujadili masuala ya utaratibu, ikiwa ni pamoja na wapatanishi gani watapewa jukumu la kujadili masuala mbali mbali ambayo yanagawa pande hizo mbili.