1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Changamoto ya usalama ni kitisho duniani

Saumu Mwasimba
17 Februari 2018

Viongozi waliokusanyika katika mkutano juu ya usalama mjini Munich wakiri kwamba dunia inakabiliwa na changamoto nyingi za kiusalama ikiwemo migogoro na ugaidi uliongezeka

https://p.dw.com/p/2sqlz
München MSC 2018 | Außenminister Sigmar Gabriel
Picha: Getty Images/AFP/T. Kienzle

Viongozi na wakuu wa nchi pamoja na maafisa wa ngazi za juu kutoka nchi mbali mbali za dunia  wanaendelea na mkutano wao muhimu juu ya usalama wa dunia katika mji wa Munich hapa Ujerumani. Waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Sigmar Gabriel aliyezungumza leo Jumamosi kwenye mkutano huo ameonya kwamba ulimwengu unakabiliwa na changamoto nyingi za kiusalama pamoja na kitisho cha kuzuka migogoro mikubwa katika kanda mbali mbali.

Waziri huyo amesema kwamba ubashiri wa mambo na uhalisia ni masuala yaliopo katika siasa za kimataifa,huku akiongeza kusema kwamba mgogoro wa Syria unaelekea mahala kunakoonesha hatari kubwa ya kuzuka vita katika upande wa  washirika wao wa karibu. Suala la mgogoro wa Korea Kaskazini limetawala mkutano huo ambapo pia waziri Gabriel amegusia kwamba kitisho kikubwa kinajitokeza katika mgogoro huo na hasa kwa kuzingatia nia ya China ya kutaka kuwa na dhima kubwa katika suala hilo,lakini juu ya hilo pia ni Urusi kutumia nguvu zake za kijeshi pamoja na kuongezeka kwa siasa za kizalendo na  siasa za ubepari yote hayo yanasababisha kitisho kikubwa duniani.

München MSC 2018 | britische Ministerpräsidentin Theresa May
Waziri mkuu Theresa May akizungumza jukwaa la usalamaPicha: Reuters/R. Orlowski

Kwa upande mwingine Waziri mkuu wa Uingereza Theresa May ambaye nchi yake inajiandaa kuuaga Umoja wa Ulaya ametowa mwito mbele ya mkutano huo wa kutafutwa mkataba mpya na Umoja wa Ulaya utakaosimamia usalama kufikia mwaka ujao ili kuhakikisha muendelezo wa ushirikiano wa kijeshi,kiintelijensia na mapambano dhidi ya ugaidi baada ya nchi hiyo kujiondoa kabisa katika Umoja wa Ulaya. Theresa May anasema ushirikiano wanaouhitaji ni ule ambao utatoa fursa kwa Uingereza na Umoja wa Ulaya ya kupata njia ya kuunganisha juhudi zao kuwa na ufanisi mkubwa pale panapohusika maslahi ya pande zote.

Kadhalika kwenye mkutano huo unaomalizika Jumapili viongozi wa Umoja wa Mataifa pamoja na Jumuiya ya Kujihami NATO wamesisitiza haja ya kusuluhisha mgogoro unaohusu silaha za kinyuklia wa Korea Kaskazini katika hotuba zao. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Anthonio Guterres ametoa wito wa kuutaka mgororo huo upatiwe suluhisho kwa njia za kidiplomasia akisisitiza kwamba hatua za  kijeshi zitasababisha maafa na matokeo mabaya.

"Ni muhimu kabisa kuendelea kuishinikiza Korea Kaskazini na kuishawishi kuja katika meza ya mazungumzo ili kuweza kupata njia ya kusitisha utengenezaji wa silaha za kinyuklia. Kuondoa silaha za kinyuklia katika rasi ya Korea inawezekana."

MSC 2018 Sergei Lawrow
Waziri wa mambo ya nje wa Urusi Sergei Lavrov akiwa mkutanoni MunichPicha: Reuters/R. Orlowski

Mbali na wasiwasi juu ya silaha za nyuklia, Guterres alionya kwamba changamoto nyingine za usalama bado zimebaki kuwepo kwa kiwango kikubwa. Katibu Mkuu huyo alisema migogoro inayoendelea katika Mashariki ya Kati kama vile vita vya nchini Syria  vinasababisha madhara hata nje ya kanda hiyo, kupitia ugaidi wa kimataifa au wingi wa idadi ya watu waliokimbia makazi yao wakikimbilia barani Ulaya na mahali pengine ulimwenguni. Kadhalika katibu Mkuu wa NATO Jens Stoltenberg aliyezungumza katika mkutano huo amerudia wito wa Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, kwa kusema shinikizo dhidi ya Korea Kaskazini lazima liendelezwe. Stoltenberg aliongeza kwamba Urusi na China zina wajibu kama nchi wanachama wa Baraza la Usalama na kama majirani wa karibu wa Korea Kaskazini.

Mwandishi: Saumu Yusuf/afp/Reuters

Mhariri: Jacob Safari