1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Chanjo zaanza kutolewa katika Umoja wa Ulaya

Iddi Ssessanga
28 Desemba 2020

Mataifa ya Umoja wa Ulaya yameanza kutoa chanjo kwa makundi ya watu katika juhudi za kumaliza janga la dunia la Covid-19. Nje ya Umoja wa Ulaya, mataifa ya Uingereza, Uswisi na Serbia, yameanza kutoa chanjo hiyo pia.

https://p.dw.com/p/3nHFl
Portugal Impstart in Krankenhäuser
Picha: Pedro Nunes/REUTERS

Mataifa ya Umoja wa Ulaya yakiwemo Ufaransa, Italia, Austria, Ureno na Uhispania yamezindua mipango kabambe ya utoaji chanjo, ambapo mataifa mengi yameanza kutoa chanjo hiyo kwa watumishi wa afya.

Utoaji chanjo katika kanda hiyo ulianza siku ya Jumapili kufuatia hatua ya mamlaka ya dawa ya Ulaya kuidhinisha chanjo ya makampuni ya BioNTech na Pfizer muda mfupi kabla ya siku ya Krismas.

Mataifa matatu ya Ujerumani, Hungary na Slovakia, yalianza, kutoa chanjo hiyo siku ya Jumamosi.

Nchini Ujerumani, maafisa waliwasilisha chanjo katika nyumba zinazohudumia wazee, ambao walikuwa wa kwanza kupokaa chanjohiuyo siku ya Jumapili.

Soma pia: Ulaya yaanza kutoa chanjo ya corona

Mbali na hospitali, kumbi za michezo na vituo vya mikutano vilivyoanchwa vitupu kutokana na hatua za karantini vitageuka maeneo ya kutolea chanjo.

Italien Impstart Senioren
Watu wakipatiwa chanjo ya Pfizer-BioNTech wakati Italia ikianza kutoa chanjo dhidi ya Covid-19.Picha: Matteo Bazzi/REUTERS

Ujerumani yenye wakaazi milioni 83, imejenga zaidi ya vituo 400 vya kutolea chanjo, ikwemo maeneo kama viwanja vya zamani vya ndege vya Tegel na Tempelhof vya mjini Berlin, na ukumbi wa maonesho ya biashara wa Hamburg.

Maafisa wa afya nchini Ujerumani walipokea dozi zao za kwanza za chanjo hiyo siku ya Jumamosi, ambapo kila moja ya majimbo 16 ya taifa hilo yalipata dozi za awali zipatazo elfu kumi.

Muuguzi wa chumba cha wagonjwa mahututi Zeynep Kallmayer, alikuwa miongoni mwa watu wa kwanza katika jimbo la Ujerumani na Hesse kupatiwa chanjo hiyo katika Hospitali ya Chuo Kikuu cha Frankfurt.

Soma pia: Nchi za Umoja wa Ulaya zapokea chanjo za kwanza za Covid-19

''Natumai watu wengi watapata taarifa za kutosha na hawatakuwa na hofu juu ya chanjo, na pia watoe mchango wao. Kwangu nachukulia kuwa ni jukumu langu kama sehemu ya jamii hii kutoa mchango wangu.''

Chanjo kupatikana kwa wote mwaka 2021

Chanjo hiyo itatolewa bure na kupatikana kwa kila mmoja kuanzia katikati mwa mwaka ujao wa 2021, wakati ambapo chanjo kwa makundi ya kipaumbele zinatarajiwa kuwa zitakuwa zimeisha. Hakuna ulaazima wa kufaniwa chanjo.

Ungarn Budapest Lieferung von Impfstoffen
Wanajeshi wa Hungary wakibeba shehena ya kwanza ya chanjo ya covid-19 katika hospitali kuu ya Del-Pest mjini Budapest, Desemba 26,2020.Picha: Szilard Koszticsak/REUTERS

Kampeni ya chanjo ya Ujerumani hata hivyo, ilikabiliwa na uchelewaji katika miji kadhaa siku ya Jumapili, baada ya kubainika kuwa karibu vichupa 1,000 vya chanjo ya BioNTech na Pfizer havikutunzwa katika baridi ya kutosha wakati wa usafirishaji.

Soma pia: WHO yakutana kwa dharura kuhusu kirusi kipya cha corona

Ufaransa, ambayo imekuwa ikirekodi karibu maambukizi mapya 15,000 kila siku katika wimbi lake la pili la janga hili, ilipokea shehena yake ya kwanza ya chanjo siku ya Jumamosi.

Maafisa wa Ufaransa walisema wangeanza kutoa chanjo hiyo katika mji mkuu wa Paris na mkoa wa Burgundy-Franche-Comte.

Nchini Italia, vibanda vya huduma ya afya vinavyotumia nishati ya jua vimepangwa kujengwa katika viwanja vya miji kote nchini kwa ajili ya kutolea chanjo hiyo.

Chanzo: Mashirika.