1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

China na Marekani zakubaliana kuhusu mambo kadhaa

17 Novemba 2009

Bado lakini viongozi hao wanatofautiana juu ya suala la haki za binadamu miongoni mwa mengine

https://p.dw.com/p/KYtl
Rais wa Marekani Barack Obama, lakisalimiana na mwenyeji wake Hu Jintao, baada ya mkutano waoPicha: AP

Rais wa Marekani Barack Obama na mwenyeji wake rais wa China Hu Jintao wamekubaliana juu ya kuimarisha uhusiano wao zaidi katika suala masuala ya uchumi,mabadiliko ya hali ya hewa,nishati na vitisho vya kinuklia kutoka nchi za Iran na Korea Kaskazini. Hata hivyo viongozi hao wawili wameonekana bado wanatofautina katika masuala ya uchumi,usalama na haki za binadamu,masuala ambayo kwa muda mrefu yamekuwa yakiutatiza uhusiano wa mataifa hayo mawili yenye nguvu. Obama ni rais wa kwanza wa Marekani kuitembelea China katika kipindi cha miaka 12.

Viongozi hao wawili wameafikiana juu ya kuimarisha uhusiano wa nchi hizo mbili na kutilia mkazo katika masuala ya uchumi,mabadiliko ya hali ya hewa nishati na Nuklia. Lakini kutokana na mazungumzo yao imedhihirika kwamba pande hizo mbili bado zinatofautiana jambo ambalo limeonyesha kwamba itakuwa vigumu kwa ziara hiyo ya kwanza ya rais Obama nchini China kumaliza mvutano na taifa hilo.Rais Obama amesema kwamba serikali ya mjini Tehran itachukuliwa hatua zinazostahili ikiwa haitothibitisha kwamba mpango wake wa kinuklia ni kwa ajili ya matumizi ya amani na kuwa wazi kuhusu mpango huo.Obama amesema Marekani na China zitashirikiana kukikabili kitisho cha Iran ikiwa itamiliki silaha za kinuklia.Pia amesema baraza la usalama la Umoja wa mataifa linazungumza kwa kauli moja dhidi ya mpango huo wa Iran.

Kwa upande wake rais Hu Jintao wa China amezungumzia zaidi juu ya diplomasia katika suala hilo la Iran ili kuimarisha usalama katika eneo la mashariki ya kati. Kuhusu Korea Kaskazini nchi zote mbili zinataka mazungumzo ya pande sita yaanze haraka iwezekanavyo.Akizungumzia hilo rais wa China alisema-

''Tumeafikiana kwa pamoja kubakia katika lengo la kuutatua mzozo wa nuklia wa Korea kaszini kupitia mazungumzo,na hatua hiyo itatuwezesha sote tunaohusika katika suala hilo kufikia lengo letu.Pande zote mbili zitafanya kazi pamoja na wahusika wengine kuendelea na mpango wa kuishawishi Korea kaskazini kuchana na harakati zake na kurudi kwenye mazungumzo ya pande sita ili kuimarisha amani na usalama katika eneo la kaskazini mashariki mwa Asia''

Barack Obama Hu Jintao China Flash-Galerie
mkutano wa rais Obama ChinaPicha: AP

lengo la pande hizo mbili katika mkutano wa Copenhagen sio kupata makubaliano ya kupendelea upande fulani au azimio la kisiasa bali wana nia ya kufikia makubaliano yatakayojumuisha masuala yote na ambayo yatatekelezwa.Akaongeza kusema kwamba-

''Nchi zetu kama watumiaji wakubwa na watoaji wa nishati hakuwezi kupatikana suluhisho katika changamoto hii bila ya juhudi zetu na ndio sababu tumekubaliana juu ya mipango kadhaa ikiwa ni pamoja na kuunda kituo cha utafiti wa nishati na kuafikiana kuhusu matumizi ya nishati isiyoharibu mazingira na pia kushirikiana kufikia mafanikio katika mkutano wa Copenhagen''

Ama kuhusu suala la Uchumi rais Obama ameitaka China kushirikiana na Marekani katika kuuongoza ulimwengu kujikwamua kutokana na mgogoro wa kiuchumi unaoendelea lakini juu ya hilo pia wamekubaliana kufuatilia ahadi zilizotolewa katika mkutano wa G20 mjini Pittsburg na kutafuta mkakati wa kuimarisha uchumi.

Hata hivyo rais wa China ameitaka Marekani kuacha mtindo wa kujipendelea katika kulinda nafasi zake za kazi, pamoja na kukataa kuitambua China kama soko kamili la kiuchumi na kudhibiti biashara ya technologia ya juu.

''Nimemsisitizia rais Obama kwamba katika hali ya hivi sasa ya kiuchumi nchi zateu zinabidi kupinga kwa dhati mtindo wa kulinda nafasi za kazi katika maeneo yote''

Na hatimae katika suala la haki za binadamu rais Obama alionekana kuchokoza nyuki aliposema kwamba makundi ya waliowachache nchini China wanabidi kupewa haki za binadamu na kuitolea mwito nchi hiyo kurudi katika meza ya mazungumzo na wajumbe wa kiongozi wa kidini wa Tibet Dalai Lama anayeishi uhamishoni. Matamshi hayo yalijibiwa kwa sauti kali na rais Hu Jintao akisema pande zote mbili zimehakikishiana juu ya msingi wa kuheshimiana na kuheshimu uhuru wa mamlaka ya kila upande Kutokana na hilo China itaendelea kuchukua hatua ya kudumisha usawa,kuheshimiana,na kutoingilia kati masuala ya ndani ya upande wa pili.