1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

China na Olimpik

5 Agosti 2008

China imeimarisha ulinzi mkali baada ya kuuwawa askari wake 16.

https://p.dw.com/p/Eqm5
Mashindano ya mashua ya olimpik.Picha: picture-alliance / dpa

Masaa 48 kabla michezo ya 29 ya olimpik mjini Beijing kufunguliwa rasmi, wenyeji China, wametangaza leo kwamba watahakikisha michezo ya usalama huku wakizidisha ulinzi mkali kaskazini-magharibi mwa China,ambako kikundi cha magaidi wa kiislamu kinaripotiwa kufanya hujuma kali ilioua askari 16 wa China. Hali ya hewa ya jiji la Beijing, imekuwa pia gumzo tangu kwa wanariadha hata kwa waandazi wa michezo hii-hali iliopelekea wanariadha kama Gebreselassie wa Ethiopia, kujitoa kukimbiab mbio za marathon.

►◄

Idara za usalama za China, zimearifu kwamba washambulizi waliowaua polisi 16 huko Xinjiang,kaskazini-magharibi mwa China,mkoa unaokaliwa na waislamu wengi na hasa wa Uighur wakitaka kuanzisha vita vitakatifu-"Jihad".Idara ya usalama ikataja kwamba kikundi hicho yamkini kina mahusiano na kile kiklicho orodheshwa na UM ambacho Beijing ilidai kinapanga hujuma juu ya michezo ya olimpik.

Licha ya hali hiyo, waandazi wa michezo ya Beijing wamejaribu kuwahakikishia wanariadha 10.000 na wageni 500.000 wanaotarajiwa Beijing kwa michezo hii kwamba, hawana haja ya kuingiwa na hofu juu ya usalama wao.

China tayari imeweka ulinzi mkali katika kila pembe ya jiji la Beijing na nchini kote.

Wakongwe wa michezo ya olimpik wameeleza kwamba ulinzi kama huo hawakuona tangu michezo ya olimpik ya Moscow, 1980.

Huko Xinjiang, mkoa unaopakana na Asia ya Kati ambako hujuma ya jana ilitokea ,waislamu wa kabila la Uighur wakilalamika kuandamwa na vikosi vya usalama vya China kwa miezi kadhaa.Wengi wao wamewekwa kizuizini.

China imetangaza usalama umeongezwa jana huko Xinjiang na hasa katika mji maarufu wa KASHGAR kulikozuka hujuma hiyo.

Polisi inasema miripuko iliotumiwa na washambulizi ni sawa na ile iliogunduliwa mwaka jana mikononi mwa Chama cha kiislamu cha East Turkestan Islamic Movement (ETIM).Hiki ni kikundi kilicho orodheshwa na UM kuwa ni cha kigaidi na ni chama kinachogombea jimbo la China la Xinjiang,ligeuke dola huru la kiislamu. Xjiang, ni jimbo lenye wakaazi milioni 8.3 wa kabila la Uighur.Wakaazi wengi wa kabila hilo wanasema hawaridhishwi na miongo kadhaa ya utawala wa mkandamizo na dhulma wa chama cha kikoministi cha China.

Mjini Beijing,baadhi ya wanariadha wameingiwa zaidi na wasi wasi na hali ya hewa kuliko usalama-hali ambayo imeselelea licha ya hatua kali zilizochukuliwa na waandazi wa olimpik.

Mwanariadha wa ki-indonesia anaebeba vyumavi zito, Syafraidi Ali amearifu kwamba kikosi chao kimepewa amri kali kutokaa nje muda mrefu.

Mwenyekiti wa Tume ya matibabu ya Halmashauri kuu ya Olimpik Ulimwenguni-IOC-Arne Ljungqvist, amesema kiwango cha kuchafuka hali ya hewa si kibaya hivyo kama ilivyohofiwa awali.Akavilaumu vyombo vya habari kutia chumvi.

Ljungqvist alidai ripoti za vyombo vya habari zimewastusha mabingwa wakubwa wa riadha kama Haile Gebrselassie wa Ethiopia na Muingereza Paula Radcliffe-mabingwa wa mbio za marathon kudhani kwamba, kushiriki katika mbio

za marathon za Beijing ni hatari kwa afya zao.