1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

China, Urusi na Iran zafanya luteka ya kijeshi

Admin.WagnerD27 Desemba 2019

Iran, China na Urusi zimeanza luteka ya pamoja ya kijeshi kwenye bahari ya Hindi na ghuba ya Oman katika kile Moscow inachosema ni zoezi lisilotarajiwa la ushirikiano wa majeshi ya majini baina ya mataifa hayo. 

https://p.dw.com/p/3VNup
RIMPAC 2014 China Zerstörer Haikou
Picha: Reuters

Zoezi hilo la siku nne lililofunguliwa katika mji wa bandari wa Chahbahar uliopo kaskazini mashariki ya ghuba ya Oman na karibu na mpaka na Pakistan linanuwia kuimarisha ulinzi katika eneo la bahari ya kanda hiyo.

Eneo la bahari linalozunguka Iran limekuwa kitovu cha mvutano wa kimataifa kufuatia Marekani kuongeza mbinyo dhidi ya mauzo na ushafirishaji wa mafuta ya Iran na kuhimiza biashara nyingine na taifa hilo zisitishwe.

Afisa mmoja wa jeshi la majini la Iran ameiambia televisheni ya taifa ya nchi hiyo kuwa ujumbe wa zoezi hilo ni amani, urafiki na ulinzi na ni ishara kwamba Iran haiwezi kutengwa kimataifa.

Kulingana na televisheni ya Iran, luteka hiyo inajumuisha meli za uokozi na mazoezi ya kufyetua makombora.

Luteka kuimarisha uhusiano wa nchi hizo

NATO Standing Maritime Group - Schwarzes Meer
Picha: Getty Images/AFP/D. Mihailescu

Hapo jana msemaji wa wizara ya ulinzi ya China Wu Qian alisema mazoezi hayo ya kijeshi yataimarisha mahusiano na ushirikiano wa majeshi ya majini miongoni mwa mataifa hayo matatu.

Kwenye mazoezi hayo China imetuma mfumo wake wa kuharibu makombora uitwao Xining wakati urusi imepeleka meli tatu za kiejshi kutoka kikosi chake cha eneo la Baltiki, mzinga wa kufyetua roketi na boti ya uokozi.

Tehran imekuwa ikitafuta kuimarisha uhusiano wake wa kijeshi na Beijing na Moscow kutokana na kishindo cha vikwazo vya kiuchumi kutoka Marekani.

Luteka hiyo inaonekana kuwa jibu dhidi ya mazoezi ya kijeshi yaliyofanywa karibuni na Marekani  pamoja na Saudi Arabia ambaye ni mshirika wake katika kanda ya Ghuba.

Luteka inafanyika kwenye eneo tete

Golf von Oman Öltanker Front Altair
Picha: picture-alliance/AP Photo/ISNA

Bahari ya Oman ambako luteka hiyo inafanyika ni eneo tete la majini kwa kuwa linaungana na mlango bahari wa Hormuz, unaopitisha asilimia 20 ya mafuta yote yanayosafirishwa duniani.

Mnamo mwezi Mei na Juni, Washington ilipendekeza kuweko kikosi cha jeshi la majini la Marekani katika kanda hiyo ili kuzisindikiza meli za mafuta kufutia mashambuliizi dhdii ya meli kadhaa za mafuta ikiwemo za Saudi Arabia.

Mvutano umeongezeka kwenye eneo hilo siyo tu kuhusu mradi tata wa nyuklia wa Iran bali pia kutokana na mashambulizi ya mwezi Sepetemba kwenye miundombinu ya mafuta ya Saudi Arabia.

China na Urusi zina uhusiano wa karibu wa kidiplomasia, biashara na nishati na Iran.

Kadhalika mataifa hayo mawili yana mahusiano mazuri na Saudi Arabia ambayo ni hasimu wa jadi wa Iran kwenye eneo la Ghuba.