1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Colombia na waasi wa FARC wafikia makubaliano mapya

Sekione Kitojo
13 Novemba 2016

Serikali ya Colombia na waasi wa FARC wamesema kwamba wamefikia makubaliano ya amani yaliyofanyiwa mapitio ili kufikisha mwisho vita vilivyodumu miaka 52. Rais Santos anatumai kuliunganisha taifa.

https://p.dw.com/p/2ScWO
Kuba Friedensabkommen Kolumbien FARC Unterzeichnung in Havanna
Picha: Getty Images/AFP/Y. Lage

Makubaliano  hayo yanakuja wiki  sita  baada  ya makubaliano  ya  awali kukataliwa  katika  kura  ya  maoni  kutokana  na  madai kwamba  makubaliano  hayo  yalikuwa  yanawapendelea  mno  waasi.

Serikali  na waasi  wa  kundi  la  Revolutionary Armed Forces , majeshi  ya kimapinduzi  ya  Colombia, FARC , ambao  wamekuwa  wakifanya mazungumzo  mjini  Havana  kwa  muda  wa  miaka  minne, wamesema wamejumuisha  mapendekezo  kutoka  kwa  upinzani, viongozi  wa  kidini  na wengine.

Kolumbien Präsident Juan Manuel Santos Rede in Bogota
Rais wa Colombia Juan Manuel SantosPicha: Reuters/Colombian Presidency

Rais Juan Manuel Santos  ana  matumaini  ya  kuliunganisha  taifa  hilo lililogawika  kwa  kutumia  makubaliano  hayo  mapya  baada  ya  hatua  za amani  kuhatarishwa  na  wananchi  kukataa  katika  kura  ya  maoni  mwezi Oktoba. Wapiga  kura  wa  Colombia  waligawanyika  kwa  kiasi  kikubwa , wengi  wao  wakiwa  na  wasi  wasi  wasi  kwamba  waasi  wa  FARC hawataadhibiwa  kwa  uhalifu  na  wengine  wakiwa  na  matumaini  kwamba makubaliano  hayo  yataimarisha  kumalizika  kwa  machafuko na  ghasia.

"Tunatoa  wito  kwa  Wakolombia  wote  na   jumuiya  ya  kimataifa  kuunga mkono  makubaliano  haya  mapya  na  utekelezaji  wake  wa  haraka  ili kuweza  kutupilia  mbali  maafa  ya  vita," pande  hizo  mbili  zilisema  katika taarifa. "Amani  haiwezi  kusubiri tena." Nakala  za  makubaliano  hayo  mapya zitasambazwa  kwa  umma  kuanzia  leo  Jumapili(13.11.2016).

Serikali  haijasema  iwapo  itafanya  kura   nyingine  ya  maoni  kuidhinisha makubaliano  hayo, licha  ya  kuwa  baadhi  ya  viongozi  wa  upinzani  tayari wanadai  kufanyika  kwa  kura  hiyo  kupitia  ukurasa  wa  Twitter.

Kuba Friedensabkommen Kolumbien FARC Unterzeichnung in Havanna
Waziri wa mambo ya kigeni wa Cuba Bruno Rodriguez Parrilla(kushoto) na mkuu wa ujumbe wa serikali katika mazungumzo ya amani na kundi la FARC Humberto de la Calle(kulia)Picha: Getty Images/AFP/Y. Lage

Makubaliano  hayo  mapya  hayajabadilisha  sehemu  tata  ya  makubaliano hayo  ambayo  yanatoa  kwa  kundi  la  FARC  viti  10  katika  bunge  la  nchi hiyo  hadi  mwaka  2026  ama  kuwazuwia  viongozi  wa  waasi  kuchaguliwa katika  nyadhifa  za  kisiasa.

Makubaliano hayataingizwa katika  katiba

Hata  hivyo , makubaliano  hayo hayataingizwa  katika  katiba  ya  Colombia na  kundi  la  FARC litatakiwa  kuwasilisha  orodha  ya vifaa  vyake  vyote  na mali, ambavyo  vitatumika  kwa  madhumuni  ya  kuwalipa  fidia waathirika, Santos  alisema  katika  hotuba  aliyoitoa  kwa  njia  ya  televisheni.

Makubaliano  hayo  yaliyofanyiwa  mabadiliko  pia  yanaondoa  majaji  wa kigeni  katika  mahakama  maalum  za  amani , licha  ya  kwamba  kutakuwa na  wachunguzi  wa  kigeni, na  kueleza  kwamba  FARC  ni  lazima  kutoa taarifa  za  kina  juu  ya  kuhusika  kwao  katika  biashara  ya  mihadarati.

Makubaliano  hayo  mapya  yanaweka  ukomo  katika  kazi  ya  mahakama maalum  hadi  miaka  10  na  yanataka  uchunguzi  wowote  kufunguliwa katika  muda  wa  miaka  miwili  ya  mwanzo.

Kolumbien Referendum Gegener des Friedensbakommens jubeln
Wapinzani wa makubaliano hayo wakiandamana kwa furaha mjini BogotaPicha: picture alliance/AP Photo/A. Cubillos

Wasi wasi  mkubwa miongoni mwa  wale  waliopiga  kura  ya  "hapana" katika makubaliano  ya  awali  ni  kwamba  waasi  waliohukumiwa  hawatatumikia kifungo  chao  jela  na  badala  yake  watafanya kazi  ya  kuondoa  mabomu  ya  kutegwa ardhini  na  kufanya  kazi  nyingine.

Haionekani  kuwa  mabadiliko  yatajumuisha  kifungo  cha  jela, lakini  Santos amesema  makubaliano  hayo  yatahakikisha  wapiganaji  wa  FARC waliohukumiwa  na  mahakama  maalum  watazuiliwa  katika  maeneo maalum, wakifanyakazi  na  utaratibu  mwingine.

Wazo la  upinzani

Wazo  la  upinzani  kwamba  viongozi  wa  FARC wasiruhusiwe  kugombea nyadhifa  za  kisiasa  mara  watakapomaliza  kifungo  chao  halikujadiliwa pamoja  na  waasi, Santos  alisema. "Hatua tulizochukua  pamoja  na  FARC sio  na  haziwezi  kuwa  za  aina  yake."

Kolumbien FARC Friedensvertrag
Wapiganaji wa kundi la FARC wakiondoka baada ya kupata taarifa kutoka kwa makamanda wao.Picha: picture-alliance/dpa/M. Duenas Castaneda

Rais  wa  zamani Alvaro Uribe , ambae  aliongoza  upande  wa  upinzani katika  makubaliano  ya  awali, hajafurahishwa  na  makubaliano  hayo yaliyofanyiwa  mabadiliko, vyanzo  vimesema. Uribe  ambaye  alikutana  na Santos , jana  Jumamosi, alisema  kambi  yake  na  waathirika  wanapaswa kupitia  makubaliano  hayo  mapya  kabla  ya  utekelezaji.

"Nimemuomba  rais  kwamba chapisho  la  makubaliano   lililotangazwa Havana  halipaswi  kuwa  la  mwisho," amesema  katika  taarifa, na  kuongeza kwamba  upinzani  huenda  ukahitaji  kufanya  mapendekezo  zaidi. Santos alishinda  tuzo  ya  amani  ya  Nobel  mwezi  uliopita kwa  juhudi  zake  za kumaliza  vita  hivyo, ambavyo  vimesababisha  watu  zaidi  ya  220,000 kuuwawa  na  wengine  wengi  kukimbia  makaazi  yao.

Mwandishi: Sekione  Kitojo / rtre

Mhariri: Sylvia  Mwehozi