1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

COVID-19 Kenya: Muda wa kutotoka nje usiku wasogezwa siku 60

28 Septemba 2020

Muda wa kutotoka nje usiku kusogezwa kwa saa moja hadi saa nne usiku kwa siku 60 zijazo. Vilabu vya pombe vitaruhusiwa kuwa wazi hadi wakati huo kuanzia Jumanne kufidia biashara waliopoteza.

https://p.dw.com/p/3j7x8
Kenia Coronavirus Uhuru Kenyatta
Picha: PSCU

Marufuku ya kutotoka nje usiku ilitangazwa kwa mara ya kwanza mwezi wa machi pale kisa cha kwanza cha corona kilipotangazwa.Shule bado hazijafunguliwa ila leo ilikuwa siku ya mwisho kwa walimu kurejea kuanza maadalizi.Kikao cha mwisho kujadili hali ya corona nchini kimefanyika alasiri hii jijini Nairobi. 

Mnamo Jumatatu kimefanyika kikao cha mwisho cha COVID 19 baada ya ripoti ya kamati ya dharura kuwasilishwa kwa Rais Uhuru Kenyatta. Kikao hicho kiliangazia mapambano dhidi ya corona na mustakabal wa nchi.

Kwenye ufunguzi rasmi wa kikao hicho cha mwisho kujadili athari za corona na mbinu za mapambano, Rais Uhuru Kenyatta alisisitiza kuwa mustakabal haujulikani ila ipo haja ya kubadili mienendo ukizingatia maambukizi. Rais alishukilia kuwa ipo haja ya kuhoji kila kilichotokea katika msimu huu.

Magavana, mawaziri na rais chini ya mwamvuli wa kamati ya dharura ya kupambana na COVID 19 wamekutana alasiri hii kwenye ukumbi wa mikutano wa kimataifa KICC. Muda mfupi baada ya ufunguzi wa kikao, Waziri wa Afya Mutahi Kagwe alimkabidhi Rais Uhuru Kenyatta ripoti maalum ya kamati ya dharura ya kitaifa ya kupambana na COVID 19.

Kongamano la leo liliwaleta pamoja viongozi wa ngazi ya juu nje na ndani ya serikali kuu.Kiongozi wa upinzani Raila Odinga aliyesindikizwa na wenzake wa mrengo huo walifika kwenye ukumbi wa KICC. Naibu wa rais William Ruto aliyetazamiwa kumkaribisha Rais Uhuru kukifungua rasmi kikao hicho hakuonekana.

Rais Uhuru Kenyatta asisitiza kuwa mustakabal haujulikani ila ipo haja ya kubadili mienendo ukizingatia maambukizi.
Rais Uhuru Kenyatta asisitiza kuwa mustakabal haujulikani ila ipo haja ya kubadili mienendo ukizingatia maambukizi.Picha: picture-alliance/AP Photo/B. Inganga

Mazungumzo yalijikita kwenye hatua zilizochukuliwa kupambana na janga la corona ukizingatia fedha zilizotumika kutoka hazina ya kitaifa na wafadhili, vifaa vya usalama, mikakati ya mapokezi ya wagonjwa mahututi, juhudi za kusaka chanjo na utafiti kwa jumla.Kwenye hotuba yake ya 11 Rais Uhuru Kenyatta aliusisitizia umuhimu wa kuiongeza kasi ya uchunguzi wa madai ya ufisadi unaodaiwa kutokea kwenye idara ya kununua dawa na vifaa vya matibabu, KEMSA.

Yote hayo yakiendelea, muda wa mwisho wa walimu kurejea shuleni umekamilika leo.Nancy Macharia ni afisa mkuu mtendaji wa tume ya kuwaajiri walimu nchini Kenya,TSC.

Walimu wanatazamiwa kuanza maandalizi ya kuwawezesha wanafunzi kurejea shuleni.Hata hivyo tarehe kamili haijakuwa bayana.Jee walimu wanahisia zipi kuhusu agizo hilo? 

Shule zilifungwa rasmi mwezi wa Machi mwaka huu baada ya kisa cha kwanza cha covid 19 kutangazwa

Mwandishi: Thelma Mwadzaya/dw Nairobi