1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

COVID-19- Vifo vyapindukia 600,000 ulimwenguni kote

John Juma
19 Julai 2020

Idadi ya vifo kutokana na janga la COVID-19 ulimwenguni imepindukia watu 600,000, hali inayoashiria jinsi ulimwengu uko mbali na matumaini ya kurejea katika hali ya kawaida.

https://p.dw.com/p/3fYW0
Coronavirus in Indien
Picha: Getty Images/Y. Nazir

Shirika la Afya Duniani WHO limerekodi takriban maambukizi mapya 260,000 ya virusi vya corona. Hiyo ni rekodi mpya ya idadi ya juu zaidi ya COVID-19 kurekodiwa ulimwenguni kote ndani ya siku moja.

Huku Marekani ikiongoza orodha ya mataifa ambayo yamerekodi maambukizi mengi zaidi, nchi ya Afrika Kusini sasa inashikilia nafasi ya tano miongoni mwa mataifa hayo, ikiwa na maambukizi 350,879. Idadi hiyo ikiwa sawa na nusu ya idadi jumla ya maambukizi yote barani Afrika

Hali katika Afrika Kusini inatizamwa kama ishara ya changamoto ambayo huenda ikazikumba nchi ambazo labda pia zina vifaa haba vya huduma za afya.

India yarekodi maambukizi mengi kwa siku moja

Katika bara la Asia, India imerekodi idadi ya juu zaidi ya maambukizi ya corona ndani ya siku moja, ya watu 38,902, hivyo kuifanya idadi ya walioambukizwa kuongezeka na kufikia watu 1, 077,618.

Kwingineko barani Asia, China imethibitisha visa vipya 13 vya maambukizi ya virusi hivyo, kaskazini magharibi mwa mji wa Urumqi. Nayo Korea Kusini kwa siku ya pili mfululizo imeripoti maambukizi ya chini ya watu 40.

Mripuko wa virusi hivyo eneo la Urumqi, ndio mripuko wa hivi karibuni nchini China, baada ya taifa hilo kuudhibiti usambaaji wa virusi hivyo katika jamii mnamo mwezi Machi.

Soma pia: Wanafunzi milioni 10 huenda wasirudi shuleni baada ya corona

Maambukizi yaongezeka Afrika Kusini

Mnamo Jumamosi, shirika la Afya Duniani WHO kwa mara nyingine liliripoti maambukizi ya juu ya watu 259,848.

Afrika Kusini ndilo taifa la kwanza la barani Afrika kuwa na idadi ya juu zaidi ya maambukizi kiasi cha kuorodheshwa miongoni mwa nchi zilizoathiriwa mno ikishika nafasi ya tano baada ya Marekani, Brazil, India na Urusi.

Mhudumu wa Afya nchini India akichukua sampuli za kufanyia vipimo kutoka kwa mvulana katika kituo cha Hyderabad mnamo Julai 17, 2020.
Mhudumu wa Afya nchini India akichukua sampuli za kufanyia vipimo kutoka kwa mvulana katika kituo cha Hyderabad mnamo Julai 17, 2020.Picha: Getty Images/AFP/N. Seelam

Mkoa wa Gauteng nchini Afrika Kusini iliyo na miji ya Johannesburg na Pretoria, ndio kitovu kipya cha mripuko huo. Robo ya idadi jumla ya raia milioni 57 wa Afrika Kusini ni wakaazi wa mkoa huo, huku wengi wakiishi katika mazingira ya msongamano wa watu.

Wakfu wa askofu wa zamani Desmond Tutu na ambaye pia ni mshindi wa tuzo ya amani ya Nobel pamoja na mke wake Leah, umeonya kwamba tatizo la Afrika Kusini ni raia wengi kutotilia maanani masharti ya Shirika la Afya Duniani ya kuepusha kusambaa kwa virusi vya corona.

Soma pia: Urusi yatuhumiwa kuiba utafiti wa chanjo ya corona

Marekani yaongoza kwa vifo na maambukizi

Jumla ya idadi ya watu walioambukizwa ulimwenguni kote imepindukia watu milioni 14.2. Watu milioni 3.7 miongoni mwao wakitokea Marekani, zaidi ya milioni 2 kutoka Brazil na zaidi ya milioni moja kutoka India.

Kulingana na takwimu za chuo kikuu cha Johns Hopkins, idadi ya watu waliofariki duniani kote kutokana na COVID-19, ni 601,549.

Marekani inaongoza idadi hiyo ikiwa imerekodi vifo 140, 119, ikifuatwa na Brazil ambayo imerekodi vifo 78,772, Uingereza imerekodi vifo 45,358 na nchini Mexico vifo 38,888.

Wataalamu wanaamini kwamba idadi ya maambukizi ulimwenguni kote ni juu kuliko takwimu zilizorekodiwa kwa sababu ya uhaba wa vipimo.

Mamilioni wahimizwa kusalia majumbani

Baadhi ya viongozi wa Umoja wa Ulaya wakati wa mkutano wa umoja huo mjini Brussels kuhusu bajeti ya kusaidia chumi zilizoathiriwa na COVID-19.
Baadhi ya viongozi wa Umoja wa Ulaya wakati wa mkutano wa umoja huo mjini Brussels kuhusu bajeti ya kusaidia chumi zilizoathiriwa na COVID-19.Picha: Reuters/F. Francois Walschaerts

Nchini Uhispania, serikali ya jimbo lenye mamlaka ya ndani Catalonia, imewahimiza takriban wakaazi wake milioni nne kusalia majumbani. Aidha imepiga marufuku mikutano ya zaidi ya watu 10 pamoja na kufunga kumbi za sinema na burudani ili kuepusha kusambaa zaidi kwa virusi hivyo. Hiyo ni baada ya maambukizi kuongezeka ndani ya wiki moja.

Wanasayansi wamepuuza matumaini ya Waziri Mkuu wa Uingereza Boris Johnson kuwa nchi yake inaweza kurejelea hali ya kawaida ifikapo Krismasi, wakisema bila ya chanjo kupatikana, haitawezekana kwa watu kurejelea maisha ya kawaida.

Viongozi wa EU wajikuna vichwa kuhusu bajeti kusaidia chumi zilizoathiriwa

Haya yanajiri mnamo wakati mkutano wa kilele wa viongozi wa Umoja wa Ulaya umeingia siku ya tatu ambapo viongozi wake wanajaribu kuafikiana kuhusu bajeti ya euro trilioni 1.85 ya kuzisaidia chumi za nchi wanachama ambazo zimeathiriwa na janga la corona.

Tayari kansela wa Ujerumani Angela Merkel ameonya Jumapili kuwa huenda mkutano huo wa kilele wa viongozi wa nchi 27 wanachama ukamalizika bila makubaliano.

(AFPE, AP)