1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Dafutari la visa Ujerumani

4 Machi 2009

Baraza la mawaziri kupitisha leo mswada wa sheria juu ya dafutari hilo.

https://p.dw.com/p/H5ba

Baraza la mawaziri la Ujerumani, linapanga leo kuidhinisha kuweka dafutari maalumu la taarifa au data za matumizi mabaya ya visa za kuingilia nchini.Shabaha yake ni kupunguza matumizi yasiostahiki ya visa kama mtindo ulivyokuwa wakati wa utawala wa serikali ya muungano ya vyama vya SPD na Kijani wa kutoa visa kiholela-holela.

Katika mswada wa sheria hii inayopitishwa leo ambayo nakala yake Deutsche welle imeipata, imetolewa kama hoja ya kupitisha sheria hiyo haja ya kuepusha kitisho kwa "usalama wa ndani wa Ujerumani".

Hatari kubwa inaoneka ipo katika kuingia watu Ujerumani kinyume na sheria na kuingiza uhalifu na ugaidi.Lawama zilizotolewa juu ya dafutari hilo, hazituwami tu kuwa taarifa mbali zitawekwa na Idara ya utawala ya shirikisho bali halkadhalika, na afisi za kibalozi hata polisi na Idara za usalama zaweza kuzitumia.

"Umekataliwa viza "au "si ruhusa kuingia nchini."Hizi ni taarifa zinazoweza kumuathiri bingwa wa komputa kutoka India aliekataliwa visa au mwsanafunzi wa fani ya kikemia kutoka China na hata pia mtumisi wa kujitolea kutoka Uganda.hii ni mifano dhahiri ya kesi zilizokwisha tokea na ambazo siku zijazo kwa msaada wa dafutari kama hilo zaweza mara kwa mara kutokea.

Mipango hii ya data la dafutari kama hizo inapingwa vikali na Shirika la Kanisa la Kiinjili nchini Ujerumani sawa linavyowaumiza kichwa baadhi ya wabunge wa vyama-tawala vya CDU na SPD Bungeni.

Kwa muujibu wa taarifa iliopata DW kutoka wizara ya ndani ya Ujerumani , katika enzi hii ya utandawazi, ni muhimu kabisa kwa jamii ya watu wa makabila mbali mbali kuwa huru na kuwa na mawasiliano ya kila aina miongoni mwa raia wa nchi mbali mbali ama kwa kutembeleana kwa jamaa za familia na kutunza mahusiano ya kufanya kazi au ya kitamaduni kuweza kuzuru Ujerumani mara kwa mara.

Hata bila ya dafutari la visa, mashirika ya misaada ya kikanisa kama vile Mkate kwa walimwengu "Brot fur die Welt" yakipata taabu watumishi wake wa misaada kuwaalika Ujerumani,seuze baada ya kupitishwa dafutari hilo-anunungunika msemaji wake wa habari Bw.Rainer Lang:

"Inapohusu kuwaalika watumishi kama hao kutoka nchi kama Somalia na Sudan,haraka huzuka shaka shaka kuwa watu hao wana azma ya kubakia hapa nchini.Na hubaki kuninginiza roho hadi dakika ya mwisho iwapo watu hao watapewa visa au la."

Kwamba serikali inabidi kuchukua hatua kuzuwia matumizi maovu ya visa ,ni jambo analolielewa uzuri Bw.Lang.Siku za nyuma kwa magengi ya wahalifu na wasafirishaji watu kimagendo anadai haikuwa shida kuwaingiza watu nchini ama kwa kazi ya ukahaba au kufanya kazi bila ruhusa .Hii inatokana kuwa 1999, serikali ya muungano ya chama chha kijamaa cha SPD na cha walinzi wa mazingira cha Kijani, iliagiza Balozi za Ujerumani kuwa maombi ya visa yazingatiwe kwa ukarimu. Sasa mpango huu unapangwa kukomeshwa kupitia dafutari hilo.