1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Darmstadt yapanda ngazi katika Bundesliga

25 Mei 2015

Msimu wa 2014 -2015 wa Bundesliga umekamilika. Na kama kawaida, siku ya mwisho ya msimu hushuhudia kila aina ya visa na vituko na hasa katika upande wa mkia wa ligi.

https://p.dw.com/p/1FWBc
Fußball 2. Bundesliga SV Darmstadt 98 vs. FC St. Pauli
Picha: picture-alliance/dpa/A. Dedert

Vitambaa vya kufutia machozi vilitumika sana katika uwanja wa Signal Iduna Park, wakati kocha Jürgen Klopp na kiungo Sebastian Kehl wakiwaambia kwaheri mashabaki.

Ilikuwa njia nzuri ya kuwaaga mashujaa hao wawili, maana Dortmund iliwazidi nguzu wapinzani wao Werder Bremen na kujikatia kibali cha kucheza katika Europa League msimu ujao. Sebastian Kehl mwenye umri wa miaka 35 aliwashukuru mashabiki wakati akijiandaa kuanza maisha mapya atakapozitundika rasmi njumu mwishoni mwa msimu huu

Ni wikendi ambayo Freiburg na Paderborn ziliiambia kwaheri Bundesliga. Lakini hamburg, watalazimika kupambana na klabu ya daraja ya pili Karlsruhe katika mchuano wa mchujo ili kujihakikishia nafasi ya kubakia katika ligi kuu. Mpambano huo wa mikondo miwili utachezwa Mei 28 na Juni mosi.

Sawa tu na ilivyokuwa katika ligi ya daraja la kwanza, pia kulishuhudiwa vita vikali katika ligi ya daraja la pili, ambapo timu tatu zililenga kupandishwa daraja katika Bundesliga. Darmstadt ilihitaji ushindi ili kupanda, na hivyo ilikamilisha kibarua hicho kwa ushindi wa moja bila dhidi ya St Pauli. Darmstadt wamewahi kucheza misimu miwili pekee katika Bundesliga: 1978-79 na 1981-82.

Mwandishi: Bruce Amani
Mhariri: Yusuf Saumu