1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Dortmund yashindwa kupanda nafasi ya tatu

Bruce Amani
30 Januari 2017

Borussia Dortmund walipoteza fursa ya kupanda hadi nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Bundesliga wakati kocha Thomas Tuchel akikabiliwa na kibarua kikali dhidi ya timu yake za zamani Mainz

https://p.dw.com/p/2WfAX
Fußball Bundesliga FSV Mainz 05 vs. Borussia Dortmund
Picha: Reuters/R. Orlowski

Dotmund ilitoka sare ya 1-1 ikiwa ni yake ya saba katika mechi 18, na wanabakia katika nafasi ya nne, pointi moja nyuma ya Eintracht Frankfurt katika nafasi ya mwisho ya tikiti ya moja kwa moja ya ligi ya Mabingwa. Matumaini yoyote ya kushindania ubingwa wa yanaokana kudidimia kwa sababu tayari BVB wako nyuma ya vinara Bayern Munich na pengo la pointi 14 na 11 nyuma ya nambari mbili RB Leipzig.

Hertha Berlin pia ilipoteza fursa ya kupanda hadi nafasi ya tatu baada ya kulazwa mbili moja na Freiburg. Kilikuwa kichapo cha nne katika mechi tano kwa vijana hao wa kocha Pal Dardai

Nambari mbili Leipzig waliwapa kichapo cha kwanza kabisa Hoffenheim msimu huu kwa kuwafunga 2-1

Vijana wa Carlo Ancelotti Bayern walisalia kileleni kwa kupata ushindi wa mabao mawili kwa moja dhidi ya Werder Bremen

Bayer Leverkusen iliduwazwa na Borussia Moenchengladbach kwa kufungwa mabao matatu kwa mawili licha ya kuwa kifua mbele 2-0. Cologne ilibakia nafasi ya saba baada ya kuinyoosha Darmastadt 6-1. Katika matokeo mengine, Ingolstadt iliishinda Hamburg 3-1, Wolfsburg ikafungwa 2-1 dhidi ya Augsburg wakati Eintracht Frankfurt iliifunga Schalke 1-0 na kusonga hadi nadi nafasi ya tatu ya msimamo wa BUNDESLIGA

Mwandishi: Bruce Amani
Mhariri: Yusuf Saumu