1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Dunia yapigwa butwaa kwa Renzi kujiuzulu

Mohammed Khelef
5 Desemba 2016

Dunia imepatwa na mshangao mwengine kwenye siasa za kimataifa baada ya Waziri Mkuu wa Italia, Matteo Renzi, kujiuzulu kufuatia kushindwa kwenye kura ya maoni, huku masoko ya hisa yakiporomoka.

https://p.dw.com/p/2TlR7
Symbolbild | Italien nach Referendum
Picha: picture-alliance/dpa/U. Zucchi

Akiwa ziarani nchini Ugiriki, Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani, ambaye huenda akawa rais wa taifa hili kubwa kabisa kiuchumi barani Ulaya, Frank-Walter Steinmeier, anasema nchi yake inatiwa wasiwasi sana na mgogoro wa kisiasa unaoiandama sasa Italia, akisisitiza kuwa ni lazima utatuliwe haraka.

"Uamuzi wa jana nchini Italia, kwa maoni yangu, unaogofya lakini ulikuwa wa wazi. Umma wa Italia umeyakataa mapendekezo ya mageuzi ya serikali ya Renzi. Jinsi mambo yanavyopaswa kuwa Italia sasa, yanapaswa kuamuliwa mjini Rome. Si jambo rahisi baada ya Renzi kutangaza kujiuzulu, lakini niseme tena kuwa huu ni mzozo wa kiserikali, si mzozo wa dola na si  mwisho wa ulimwengu wa kimagharibi, lakini pia si maendeleo mazuri kwa mgogoro mzima wa Ulaya, kiujumla," aliwaambia waandishi wa habari mjini Athens.

Wakati Steinmeier akijaribu kuzitenganisha athari za mzozo huo na hali halisi ndani ya bara la Ulaya, masoko ya hisa hayaoni hivyo, kwani muda mchache tu baada ya Renzi kutangaza uamuzi wake wa kujiuzulu, hisa ziliporomoka vibaya kwenye masoko ya Ulaya.

Italien Premierminister Matteo Renzi und die 'Ja' Kampagne in Florenz
Kampeni za Matteo Renzi kutaka madaraka makubwa zaidi kwa serikali kuu hazikukubaliwa na wapigakura.Picha: picture-alliance/abaca/C. Bressan

Mjini Milan, kulirikodiwa anguko la asilimia mbili, ingawa taarifa za kushindwa kwa mgombea urais wa mrengo mkali wa kulia nchini Austria zilikuwa zimeanza kulipa uhai soko hilo. 

Uamuzi wa wapigakura wa Italia umeiporomosha sarafu ya euro hadi kwenye thamani ya dola 1.056, kikiwa ni kiwango cha chini kabisa kuwahi kutokea tangu mwezi Machi mwaka jana. Hata hivyo, masoko ya hisa mjini Frankfurt, Paris na London yanaripotiwa kutikisika kidogo sana asubuhi ya leo, na baadaye kurudi kwenye nafasi yake ya kawaida. 

Hali kama hii ya masoko ya hisa kutikisika kutokana na maamuzi ya wapigakura, ilishuhudiwa pia mara mbili mwaka huu - kwanza mwezi Julai baada ya Waingereza kuamua kujiondoa kwenye Umoja wa Ulaya kwenye kura ya maoni ya Brexit na kisha mwezi Novemba, baada ya Wamarekani kumpa ushindi mkubwa mgombea urais wa Republican, Donald Trump.

Rais Mattarella ataka utulivu

Äthiopien italienischer Präsident Sergio Mattarella
Rais Sergio Mattarella anataka sasa raia watulie kungojea uamuzi wa kisiasa wa viongozi wao, wakati nchi ikipitia kwenye mkwamo wa kisiasa.Picha: Getty Images/AFP/Z. Abukeker

Hayo yakiendelea, mjini Rome kwenyewe, Rais Sergio Mattarella, ametoa wito wa utulivu, mara tu baada ya Renzi kutangaza kujiuzulu. Shirika la habari la ANSA linasema rais huyo ambaye asubuhi ya leo alikuwa na mazungumzo kwa njia ya simu na Renzi, alitaka watu wangojee maamuzi ya kisiasa, kwani "nchi inahitaji mazingira ya kisiasa kuwa ya utulivu na kuheshimiana."

Asilimia 59 ya wapiga kura wameukataa mpango wa kuifanyia mabadiliko katiba ya nchi yao, ambao ulitaka kuyaweka madaraka makubwa kwenye serikali kuu na ambao ulikuwa ukipigiwa chapuo na Renzi. Idadi ya waliojitokeza kupiga kura ni asilimia 65.5 na hivyo kulifanya anguko la Renzi kuwa kubwa zaidi. 

Sasa taifa hilo kubwa kwenye pwani ya Bahari ya Kati linakabiliwa na moja kati ya mawili: ama chama cha Renzi cha PD kiunge mkono kundi lenye wajumbe wengi bungeni na kuunda serikali ya mpito, ama kuitishwa kwa uchaguzi mpya.

Muungano wa vyama vya upinzani vinavyopingana na Umoja wa Ulaya, M5S, unashinikiza uchaguzi wa mapema, huku Renzi mwenyewe akiondoa kabisa uwezekano wa kubakia kuongoza serikali ya mpito kuelekea uchaguzi huo.

Mwandishi: Mohammed Khelef/AFP/dpa
Mhariri: Saumu Yussuf