1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Duru mpya ya kombe la klabu bingwa Afrika

14 Februari 2008

Duru mpya inaanza ya kombe la klabu bingwa na Zamalek inataka kuigiza timu ya taifa kutwaa pia ubingwa.

https://p.dw.com/p/D7Yl

Wiki tu baada ya kuziteka timu za taifa za bara zima la Afrika kwa kiatu cha kabumbu, Misri inalenga mkuki wake sasa kutwaa kombe la klabu bingwa barani afrika:

Na kinyan’ganyiro cha kombe hilo kinaanza mwishoni mwa wiki hii kikiingiza mapambano 24 ya duru ya kwanza.Miongoni mwa mabingwa 6 wa zamani watakokua uwanjani ni Zamalek ya Misri.

Wakiwa mahasimu wakubwa nyumbani Cairo wa mabingwa mara kadhaa Al Ahly, Zamalek wanajivunia mshambulizi hatari alietamba katika kombe la Afrika la mataifa huko Ghana Amr Zaky, wengine ni Hosny Abd Rabou na Aboutrika –ufunguo wa ushindi wa Misri wa Kombe la Afrika la mataifa.

Kipa wapili wa Misri-Mohamed Moncef na beki mshahara Mahmoud Fathallah na Tarek al-Sayed ni wachezaji wengine wa Zamalek katika kimkosi cha mafiraouni kilichotoroka na kombe Ghana hadi Cairo majuzi.

Ni majogoo hao wa zamalek ambao APR ya Rwanda inajiwinda kuwazim,a mwishoni mwa wiki.

Zamalek imelitwaa kombe hili jumla ya mara 5.Kikosi cha APR ni mchanganyiko wa mastadi wa nyumbani na wale wa nchi jirani imeziaibisha hatahivyo timu kadhaa zenye majina makubwa kama zamalek katika uwanja wao wa Taifa wa Amahoro miaka ya karibuni.

Miongoni mwa mabingwa wengine wanaoania kombe hili ni Club Africain ya Tunisia waliotamba 1991,Entente Setif ya Algeria (1988),Enyimba ya Nigeria iliowika 2003 na tena 2004,FAR Rabat ya Morocco-mabingwa 1985 na Hearts of Oak ya Ghana-mabingwa 2000.

Club Africain inayorejea katika kinyan’ganyiro hiki baada ya kupita miaka 11 inakumbana na Saloum ya Senegal inayoania kombe hili mara ya kwanza.Hearts of Oak inapambana na FC 105 ya Gabon . Africa Sports wanawatembelea wanagenzi wengine katika kombe hili Tonnerre ya Bennin.

Kamerun ambayo haikutoa klabu bingwa barani Afrika tangu pale Canon Yaounde ilipolinyanyua kombe miaka 28 iliopita.

Conton Sport Garoua na Union Douala ndizo zinaiwakilisha Kamerun mwaka huu na zote zinaanza n’gambo-moja dhidi ya Vital’o ya Burundi na nyengine inapambana na ASKO Kara ya Togo.

Mamelodi Sundowns,timu ya mwisho ya Afrika kusini kutamba katika Kombe la Afrika la klabu bingwa ilipoibuka makamo-bingwa nyuma ya Alahly 2001,itaitembelea Miembeni huko Zanzibar.Timu ya pili ya afrika Kusini Platinum Stars,inaikaribisha timu ya Lesotho-Correction service wakati kikosi cha polisi cha Swaziland-Royal Leopards wanawakaribisha makamo-bingwa wa 1998 Dynamo ya zimbabwe.

Miongoni mwa timu zilizoingizwa moja kwa moja duru ya pili, ni mabingwa watetezi-Etoile du Sahel ya Tunisia ilioitimua Al Ahly ya Misri kwa mabao 3-1 desemba mwaka jana ili kuvaa taji.kwa ushindi ule iliizuwia Al Ahly kuvaa taji kwa mara ya 3 mfululizo.Msimu huu Etoile itakua na jukumu kuzuwia klabu ya Misri kuigiza timu ya taifa kuibuka mabingwa wa Afrika pande zote mbili.