1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

DW inatengeneza video zenye habari kwa Kiswahili

19 Aprili 2016

Idhaa ya Kiswahili ya DW imeanzisha huduma mpya iitwayo "Papo kwa Papo" ya kusambaza video fupi ya habari kupitia mitandao ya kijamii.

https://p.dw.com/p/1IXvJ
Kiswhahili Redaktion Papo kwa Papo
Timu ya waratibu wa mitandao ya kijamii ya Dw, wakati ikipeperusha hewani video ya kwanza ya Papo kwa Papo 19.04.2016Picha: DW

Idhaa ya Kiswahili ya DW imeanzisha huduma mpya: Mukhtasari wa habari ndani ya sekunde 100. Mbali na kukuletea matangazo ya redio ya kila siku kwa ajili ya Afrika Mashariki na eneo la Maziwa Makuu, Jumatatu hadi Ijumaa DW itakupatia video fupi zenye habari. Mkuu wa Idhaa ya Kiswahili, Andrea Schmidt, ana furaha kwamba yeye na timu yake ya waandishi wa habari kutoka nchi tano tofauti wanaanzisha huduma hii mpya itakayoitwa “Papo kwa Papo” na itakayokuwa jicho la kuutazama ulimwengu. Kupitia video zetu utaweza kupata habari muhimu za kimataifa za kila siku.

“Papo kwa Papo” itapatikana katika chaneli ya YouTube ya DW Kiswahili, Facebook na toleo fupi la sekunde 60 litarushwa kupitia WhatsApp.

Miongoni mwa mambo mengine, tutakuletea “hashtag” zilizovuma pamoja na katuni za kisiasa kutoka kwa wasanii maarufu Gado na Said Michael.

Pamoja na hayo, kila Ijumaa DW Kiswahili itakuletea sekunde 100 za matukio muhimu ya kisiasa yaliyotokea katika juma zima.

· Tafadhali kuwa shabiki wetu YouTube: www.youtube.com/kiswahili

· Jiunge nasi katika ukurasa wetu wa Facebook: https://www.facebook.com/dw.kiswahili.

· Pata “Papo kwa Papo” na taarifa zaidi kupitia WhatsApp. Unaweza kujiunga nasi kupitia kiungo hiki: bit.ly/1Q86kjt

Schmidt Andrea Kommentarbild App
Mkuu wa Idhaa ya Kiswahili ya DW Andrea Schmidt

Kila siku Idhaa ya Kiswahili ya DW inarusha masaa matatu ya matangazo Afrika Mashariki na katika eneo la Maziwa Makuu. Kwa kushirikiana na redio washirika katika eneo zima, DW inawapatia wasikilizaji habari zisizoegemea upande wowote kuhusu yanayojiri duniani kwa ujumla na hasa barani Afrika kupitia masafa ya FM. Ili kutoa mtazamo huu wa kimataifa, timu ya waandshi wa habari kutoka nchi tano inafanya kazi na mtandao mkubwa wa waandishi walioko Afrika na kwengineko.

Matangazo ya Kiswahili ni miongoni mwa matangazo ya DW yenye wasikilizaji wengi zaidi. DW inajumuisha vipindi vilivyopokea tuzo kama vile Learning by Ear - Noa bongo, jenga maisha yako - na vipindi vinavyojadili afya, haki za binadamu, mazingira, wanawake na maendeleo, vijana na utamaduni na sanaa.

Maoni ya wasikilizaji na mashabiki

Baadhi ya wafuatiliaji wa matangazo ya Idhaa ya Kiswahili ya DW waliokuwa wa kwanza kuitama vidio ya Papo Kwa Papo leo wameandika maoni yao katika ukurasa wetu wa Facebook.

Anaclet Anatory Feruzi anasema DW mnatisha, wengine wakasome. hili ni funzo kwa wengine.

Mbaga Karim anasema hii ni habari njema kwetu sisi wasikilizaji wa DW tunaofuatilia habari zenu za kila siku. DW mnavuma kwa kishindo!

Katoto Ever - Kwanza natumia fursa hii kuwapongeza DW kwa mapinduzi makubwa haya ya habari pia asanteni. Nami nafurahi kuwa mmoja kati ya wale waliokuwa wa kwanza kuchangia kwenye huduma hii.

Dismas Komba wa Ifakara Morogoro Tanzania anasema hongera DW kwa kuwa nasi kwa karibu wasikilizaji wenu ama kweli DW hakuna mpinzani

Clifford Hezron Mwana Nyanda anasema hakika kwa sasa DW inazidi kupanuka kila uchao.

Thobias Yohana sijui niseme nini jinsi mnavyonifurahisha!

Mwl Nicholaus Makoye wa Chato, Tanzania amesema shaka mafanikio ya DW yanaonekana kwa sababu ya kuwa wataalamu wazuri wa mambo ya uandishi.

Tafadhali uendelee kupata huduma hii kila siku kuanzia sasa.

Mwandishi: Andrea Schmidt
Tafsiri: Elizabeth Shoo
Mhariri: Josephat Charo