1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

FIFA yakataa kuongeza timu kombe la dunia

Lilian Mtono
23 Mei 2019

Shirikisho la soka duniani, FIFA limekataa kuongeza idadi ya timu zitakazoshiriki kwenye michuano ya kombe la dunia ya  2022 huko Qatar, kutoka timu 32 hadi 48 kama ilivyopendekezwa.

https://p.dw.com/p/3IviA
Schweiz Zürich FIFA Logo am Hauptquartier
Picha: picture-alliance/dpa/S. Schmidt

Kwenye taarifa yake, FIFA imesema baada ya majadiliano ya kina na wadau wote muhimu, imeamua kwamba chini ya mazingira ya sasa haitaweza kulitekeleza pendekezo hilo kwa wakati huu.

Michuano hiyo sasa itasalia na timu 32 za awali na hakutakuwa na pendekezo litakalowasilishwa kwenye kongamano lijalo la FIFA litakalofanyika Juni 5. Maamuzi hayo ya mwisho ya FIFA yametolewa mapema tofauti na ilivyotarajiwa kwamba yangetolewa wakati wa kongamano hilo litakalofanyika Paris, Ufaransa kabla ya michuano ya kombe la dunia ya wanawake.  

Rais wa FIFA, Gianni Infantino aliunga mkono pendekezo hilo, na maamuzi haya yanatajwa kuwa pigo kubwa kwake. 

Kulingana na FIFA pendekezo la kuongeza idadi ya timu kwa muda mrefu limekuwa ni suala tete, na zaidi kwa wenyeji wa michuano hiyo Qatar, ambayo inakabiliwa na vikwazo kutoka kwa Saudi Arabia , Umoja wa Falme za Kiarabu pamoja na washirika wao.