1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mwanariadha Gatlin atimka kwa muda wa kasi zaidi

29 Juni 2015

Kikundi imara na chenye ari kubwa cha wanariadha wa mbio fupi wa Marekani kimejiandaa vilivyo kumaliza ukame wa muda mrefu wa kutopata mafanikio makubwa katika mashindano ya kimataifa

https://p.dw.com/p/1FpjJ
Leichtathletik Justin Gatlin Sieger
Picha: picture alliance/dpa/J. Warnand

Taifa hilo ambalo wakati mmoja liliwahi kutawala mbio fupi, halijashinda taji la kimataifa katika mbio za mita 100 tangu mwaka wa 2007, lakini huenda hilo likabadilika katika mashindano ya ubingwa wa ulimwengu ya IAAF mjini Beijing mwezi Agosti. Kikiongozwa na mwanariadha wa kasi zaidi Justin Gatlin, kikosi cha Marekani kilichotajwa mwishoni mwa wiki baada ya kufanyiwa majaribio kimejaa vipaji ambavyo vinaweza kuubadilisha ulimwengu.

Gatlin aliwasilisha ujumbe kwa wapinzani wake wakiongozwa na Usain Bolt, kwa kushinda taji la mita 200 katika mashindano ya riadha ya Marekani kwa kutumia muda wa kasi zaidi wa 19.57. Rekodi hiyo imeifuta ile ya sekunde 19.68 aliyoiweka mnamo mwezi Mei katika mashindano ya Eugine Diamond League, wakati huo ikiwa rekodi bora duniani.

Gatlin mwenye umri wa miaka 33, ambaye alikamilisha mnamo mwaka wa 2010 adhabu ya kufungiwa kushiriki mashindanoni kwa miaka minne, sasa ni mwanariadha wa tano wa kasi zaidi katika mbio za mita 200, nyuma ya Usain Bolt – anayeshikilia rekodi ya ulimwengu ya 19.19 – Yohan Blake, Michael Johnson na Walter Dix.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/Rueters
Mhariri: Iddi Ssessanga