1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

GAZA CITY : Haniyeh anusurika kuuwawa

15 Desemba 2006
https://p.dw.com/p/CCj8

Kundi la Hamas linalishutumu kundi hasimu la Fatah la Rais Mahmoud Abbas wa Palestina kwa kujaribu kumuuwa Waziri Mkuu Ismael Haniyeh wa serikali ya Palestina inayoongozwa na kundi hilo.

Msafara wa Haniyeh ulizuiliwa kwa masaa kadhaa katika kituo cha ukaguzi cha mpakani cha Rafah baada ya waziri mkuu huyo kujaribu kuingia katika ardhi ya Palestina na mamilioni ya dola zikiwa ni fedha taslimu akijaribu kukwepa vikwazo vya kimataifa.

Baada ya kuziacha fedha hizo kwa wasaidizi wake nchini Misri msafara wa Haniyeh ulikuja kushambuliwa baada ya kuvuka mpaka na kuingia Gaza.Mmojawapo ya walinzi wa Haniyeh aliuwawa na mwanawe wa kiume kujeruhiwa katika mashambuliano ya risasi kati ya walinzi wa mpakani wa kundi la Fataha na walinzi wa usalama wa Hamas.

Rais Mahmoud Abbas ameelezea masikitiko yake juu ya tukio hilo lakini amekanusha kuhusika kwa aina yoyote ile kwa walinzi wa Urais katika mashambulizi hayo.