1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

GAZA : Israel imeendelea kushambulia Gaza

27 Mei 2007
https://p.dw.com/p/CBxq

Israel imeendelea na mashambulizi yake ya anga huko Gaza hapo jana na kuuwawa wanamgambo watano wa Hamas na kumkamata waziri mwengine wa serikali ya Palestina katika Ukingo wa Magharibi wakati wanamgambo wa Gaza wakivurumisha makombora zaidi kwa Israel.

Wanajeshi wa Israel pia wamewauwa kwa kuwapiga risasi wapiganaji wawili wa Kipalestina baada ya wapiganaji hao kuwafyetulia risasi wanajeshi hao huko Jerusalem ya Mashariki. Katika shambulio hilo Waisrael wawili wamejeruhiwa mmoja akiwa katika hali mbaya.

Maafisa wa Israel wanasema mashambulizi yao ya anga yamelenga majengo manne yanayotumiwa na wizara ya ulinzi ya Palestina ambayo inadhibitiwa na kundi la wanamgambo wa Hamas.

Waziri alietiwa mbaroni ni Wasfi Qubaha ambaye ni waziri wa nchi na alikamatwa na wanajeshi wa Israel akiwa nyumbani kwake kwenye mji wa Jenin kaskazini mwa Ukingo wa Magharibi.

Anakuwa waziri wa pili wa kundi la Hamas kutiwa mbaroni na Israel katika kipindi cha siku tatu zilizopita.