1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Gereza la Guantanamo kuwa historia karibuni

Sekione Kitojo19 Desemba 2008

Wakati serikali mpya ya Marekani itakapoingia madarakani itahakikisha kuwa gereza la Guantanamo litakuwa historia kama anavyosema waziri wa sasa na wa baadaye wa ulinzi nchini humo Robert Gates.

https://p.dw.com/p/GJaE
Waziri wa ulinzi wa Marekani Robert Gates akihutubia mkutano wa kimataifa wa usalama wa mikakati ya kimkoa mjini Manama, Bahrain hivi karibuni.Picha: AP

Kufuatia mabadiliko ya serikali nchini Marekani waziri wa ulinzi wa nchi hiyo Robert Gates , ambaye atakuwa anaendelea na wadhifa huo katika wizara hiyo wakati rais mteule Barack Obama atakapoingia madarakani , amewataka maafisa wake kutayarisha mpango wa kulifunga gereza la Guantanamo nchini Cuba. Mashirika ya kutetea haki za binadamu yamekuwa yakidai mara kwa mara miaka kadha iliyopita kufungwa kwa gereza hilo, ambalo limekuwa likiwahifadhi watuhumiwa tangu pale baada ya shambulio la kigaidi la Septemba 11, 2001 bila ya watuhumiwa hao kufikishwa mahakamani.



Kwa mara ya kwanza waziri wa sasa wa ulinzi na ambaye ataendelea kuwa waziri katika wizara hiyo Robert Gates amesema wazi bila ya kusita. Nataka kulifunga gereza la Guantanamo, na hii itakuwa haraka iwezekanavyo.

Robert Gates ameyasema hayo katika mahojiano na televisheni ya Marekani ya PBS. Katika wakati huu inaonekana kuwa waziri huo wa ulinzi ana mawazo sawa na rais mteule Obama.

Katika mazungumzo yao na Obama , ametambua kuwa kufungwa kwa gereza hilo la Guantanamo ni suala muhimu lenye umuhimu wa juu kwa rais huyo mteule. Na pia kwa serikali yote ya rais Obama.

Itachukua muda gani hadi kufungwa kwa gereza hilo, suali hilo hakuweza kulitolea jibu sahihi waziri huyo atakayekuwa pia katika serikali ya rais Obama. Inawezekana wafungwa 50 kati ya wafungwa wapatao 250 ambao wanashikiliwa katika gereza hilo wataachiliwa haraka iwezekanavyo, kwa kuwa kwa muda wa miaka kadha wameonekana kuwa hawana hatia. Lakini hakuna nchi inayotaka kuwachukua watu hao. Inabidi kuendelea kutafuta nchi ambayo itakuwa tayari kuwachukua watu hao, amesisitiza waziri huyo wa ulinzi wa Marekani.

Ukweli ni kwamba , hatujapata nchi ambayo itawachukua. Na hususan tunataka kuwa na uhakika kuwa watu hao hawatakamatwa tena na kuteswa.


Gates amewataka maafisa wake katika wizara hiyo kutoa pendekezo jinsi ya kulifunga gereza hilo, kile kitakachohitajika ili kuweza kulifunga, na kuwaondoa wafungwa kutoka katika gereza hilo, wakati huo huo , wakihakikisha usalama wa watu wa Marekani kutokana na baadhi ya wafungwa ambao ni hatari.

Obama ameahidi kulifunga gereza la Guantanamo, ambalo limekuja kuwa alama ya matumzi ya nguvu katika kuwafunga watu , ambapo imesababisha Marekani kushutumiwa kwa madai ya utesaji.

Naamini uwezo wa mahakama za Marekani pamoja na usalama wa jela zake.

Hayo amekuwa akiyasisitiza kila mara Obama wakati wa kampeni za uchaguzi.

►◄