1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ghana yaipiga kumbo Morocco 2:0

29 Januari 2008

Morocco na Namibia zimeaga kombe la Afrika la mataifa wakati Ghana na Guinea zimeingia duru ijayo.

https://p.dw.com/p/CzFG

Katika kombe la Afrika la mataifa nchini Ghana, Ivory Coast wana miadi leo na Mali mjini Accra kukata tiketi yake ya robo-finali wakati Nigeria,hatima yao haimo mikononi mwao hata ikiitimua nje leo Benin.

Jana, Ghana na Guinea-timu 2 zilizofungua dimba la kombe hili la 26 la Afrika Januari 20, zilikata tiketi zao za duru ijayo ya robo-finali baada ya Black Stars kuizaba Morocco mabao 2-0 wakati Guinea ikihitaji suluhu tu ya bao 1:1 na Namibia kuingia duru ijayo.

Hatima ya Nigeria na kocha wao mjerumani berti Vogts itajulikana leo Nigeria ikiania pointi 3 kutoka kwa Benin na Mali ikihitaji alao suluhu na Corte d’Iviore ili kuipiga kumbo Nigeria.

Ivory Coast na mali zote mbili zina hamu leo kuepuka mkutano na wenyeji Ghana mjnini Accra jumapili hii ,baada ya Black Stars kuparamia jana kilelelni mwa kundi A.

Kwahivyo, suluhu kati ya Corte d’Iviore na Mali itahakikisha Corte d’Iviore inaibuka kileleni mwa kundi B na kupanga miadi na Guinea mjini Sekondi jumapili na kuifungulia Mali mlango wa robo-finali duru ijayo.Hii itaipiga kumbo nje ya mashindano haya Nigeria hata ikiwa leo itaishinda Benin-jambo ambalo lazima Nigeria ifanye kwa kila hali na kutumai Ivory Coast inawaokoa kwa kuitoa Mali.

Akishambuliwa na mashabiki kuwa hana lake jambo, kocha wa Nigeria,Berti vogts zamani kocha wa timu ya taifa ya Ujerumani na Scotland amejipatia imani ya shirikisho la dimba la Nigeria (NFA) licha ya kwamba Nigeria imekumbwa na misukosuko katika kombe hili la Afrika na imevuna pointi 1 tu kutoka mechi 2.Mwenyekiti wa chama cha mpira cha Nigeria Sani Lulu amewaambia maripota kwamba Vogts ndie kocha bora kabisa kwa timu ya Nigeria na hana lawama kwa kutocheza uzuri kwa Super Eagles huko Ghana.Yafaa kwahivyo kusubiri na kuona iwapo imani ya shirikisho la dimba la Nigeria kwa Berti Vogts itabaki baada ya firimbi ya mwisho kulia ya mpambano wa leo na Benin na Ivory Coast na Mali.

Jana Ghana iliparamia kileleni mwa kundi A baada ya kuipiga kumbo Morocco kwa mabao 2 –moja la Michael Essien na jengine la Sulley Muntari.Stadi wao wa kiungo Essien wa Chelsea sio tu alitia bao jana katika lango la simba wa atlas bali aliandaa bao jengine kwa Muntari kulifumania lango la wamorocco walioanza kombe hili kwa vishindo vikubwa kwa kuichapa namibia mabao 5-1.Ilikua lakini Muntzari alieandaa bao la kwanza na kumlishia dimba Essien kabla Essien nae kurejesha ukarimu kwa Muntari.Kocha wa Morocco mfaransa Henri Michel, alieiongoza Core d’Ivire katika finali ya kombe lililopita la Afrika mjini cairo alisema baadae na ninamnukulu,

„sasa inatupasa kuangalia mbele na kujenga kikosi kipya.“ Kwani, hii ni mara ya pili mfululizo kwa Morocco kupigwa kumbo katika duru ya kwanza ya kombe hili.

Licha ya kutoka sare bao 1:1 na Namibia, Guinea ilikamilisha mpambano wake wa mwisho jana na namibia ikiwa na pointi 4 –moja zaidi kuliko Morocco.Souleymane Youla aliufum,ania mlango wa namibia mnamo dakika ya 62 ya mchezo baada ya hodi hodi nyingi bila kuitikiwa.Namibia ikipigania kutorudi Windhoek mikono mitupu, ilichachamaa na kusawazisha dakika 11 baadae kwa bao la pili katika mashindano haya la Brian Brendell.

Inavyoonesha kwa sasa Ghana,Guinea zimeifuata Ivory Coast katika robo-finali ya kombe hili.