1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

GHAZNI: Kundi la Taliban lafikia makubaliano na serikali ya Korea Kusini

28 Agosti 2007
https://p.dw.com/p/CBV0

Wanamgambo wa kundi la Taliban nchini Afghanistan na maafisa wa serikali ya Korea Kusini wamefikia makubaliano ya kuachiliwa huru mateka wa rehani raia wa Korea Kusini ambao wamekuwa wakizuiliwa na kundi hilo kwa zaidi ya mwezi mmoja.

Mpatishi wa kundi la Taliban ambaye hakutaka jina lake litajwe, amesema serikali mjini Seoul imekubali kuondoa wanajeshi wake walio nchini Afghanistan na makundi ya wamisionari wa kikristo kufikia mwisho wa mwaka huu.

Serikali ya Korea Kusini mjini Seoul imelikaribisha tangazo hilo lakini ikasema haijajua ni lini hasa mateka hao watakapoachiwa. Hata hivyo, msemaji wa rais Roh Mo- Hyun wa Korea Kusini, ameonya huenda ikachukua muda kabla mateka hao kuachiliwa huru.

Wakati huo huo, hakujakuwa na taarifa yoyote kuhusu mhandisi mjerumani aliyetekwa nyara na wanangambo wa Taliban mwezi uliopita.