1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Gonzales mwishoe ajiuzulu

28 Agosti 2007

Mwanasheria mkuu wa Marekani ameitikia shinikizo na mwishoe ametupa taula ringini-amejiuzulu.Rais Bush amtetea kuwa akipakwa matope bure.wapinzani wanadai ndie mtungaji mikakati ya vita dhidi ya ugaidi na hata gereza la guantanamo:

https://p.dw.com/p/CH90
Gonzales an'gatuka
Gonzales an'gatukaPicha: AP

Mwanasheria mkuu wa serikali ya Marekani Alberto Gonzales, mwishoe aliitikia jana shinikizo la kumtaka ajiuzulu.

Kipindi chake madarakani, kilikumbwa na visa kadhaa vya kashfa kuhusu uaminifu wake na kupelekea chama cha upinzani cha Democrat kudai achunguzwe.

Rais George Bush,alibidi shingo upande kuridhia hapo jana Gonzales ajiuzulu.

Alberto Gonzales,ndie mtungaji wa mikakati ya mfululizo ya kupiga vita ugaidi,mbinu za kisheria lakini pia ndier alieongoza kutimuliwa kwa washtaki kadhaa wa serikali na kufika hadi kupoteza imani ya wafuasi wengi wa chama chake cha Republican.

Gonzales ni mshirika mwengine wa chanda na pete wa rais Bush anaeacha marekebu inayoenda mrama-wiki 2 tu baada ya Karl Rove, kigogo cha siasa nyuma ya rais Bush kumuacha mkono.Pia hii inatokea miezi 17 kabla ya nahodha mwenyewe rais George Bush,kuondoka ikulu-White House.

Akimtetea hadi dakika ya mwisho mwanasheria wake mkuu, rais George Bush alimueleza Gonzales: “Gonzales ni mtu wa kuheshimika,mwenye utu na akifuata kanuni zake za kimsingi,ispokuwa jina lake likipakwa matope kwa sababu za kisiasa.”

Alimtetea rais Bush wmwanasheria wake mkuu.

Wapinzani wake na wengi kutoka chama cha Upinzani cha democrat, wamedai afanyiwe uchunguzi wa kibunge juu ya jinsi alivyoendesha wizara yake ya sheria na Ikulu.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya sheria ya Baraza la Senate Patrick Leahy, alisema kuwa Gonzales aliigeuza wizara ya sheria “chombo cha kisiasa cha kutumiwa na Ikulu ya Marekani-White House.”

“Kwa zaidi ya miezi 6 wizara ya sheria imekua katika mtafaruku.Kwani, mwanasheria mkuu wa serikali aliongoza kufukuzwa kwa wanasheria kadhaa tena kwa sababu za kisiasa.Na akiongoza wizara hii chini ya misingi ya nadharia za kisiasa na sio chini ya misingi ya kisheria.”

Seneta mwengine kutoka chama cha Democrat Chuck Schumer aliongeza na ninamnukulu,” Chini ya Alberto Gonzales,wizara ya sheria ilikua meli inayozama.”

Lakini Seneta John Cornyn wa chama tawala cha republican, alimtetea Gonzales,kutoka Texans kama yeye aliposema,

“Ni aibu kuona mtu mwema anateketezwa katika mabishano ya kichama mjini Washington DC ingawa hakufanya lolote bayakama ushahidi utavyoonesha.”

Binafsi Robert Gonzales, alisema: “Hata siku zangu mbaya kabisa kama mwanasheria mkuu,zilikuwa bora kuliko siku nzuri za baba yangu.”

Wanaomkosa mno ´Gonzales,mshauri wa zamani wa Ikulu, wanadai ni yeye alieidhinisha mitindo ya kuwatesa wafungwa wakati wa kuwahoji katika vita dhidi ya ugaidi.Pia akiidhinisha mipango kama ya kunasa mazungumzo ya simu ambayo ikikiuka katiba ya Marekani.

Ni yeye aliedai kuwa wale washukiwa ugaidi waliowekwa korokoroni huko Guantanamo,kisiwani Kuba hawana haki ya kujitetea chini ya mapatano ya Geneva juu ya wafungwa.

Isitoshe, ametuhimiwa na chama cha upinzani cha Democrta kuwafukuza washatki 8 wa serikali chini ya misingi ya kisiasa-hatua ambayo ilipalilia mlolongo wa vikao vya bunge kusikiliza mashtaka na kulizusha mvutano mrefu baina ya Ikuku na Bunge.