1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Gulu, Uganda. Majeshi ya serikali na waasi vidole viko tayari kufyatua risasi.

5 Oktoba 2006
https://p.dw.com/p/CD5s

Kuvunjika kwa uaminifu baina ya serikali ya Uganda na waasi wiki kadha baada ya kutiwa saini makubaliano ya kihistoria ya kusitisha mapigano kumeziacha pande hizo mbili kukaribia kupigana tena na kuyaingiza mazungumzo ya kumaliza moja kati ya vita virefu barani Afrika katika hatari ya kuvunjika.

Waasi wa Lords Resistance Army walitia saini makubaliano ya kihistoria ya kusitisha mapigano na serikali mwezi wa August ambapo wengi walikuwa na matumaini kuwa yatasitisha vita vya kikatili vya miaka 20 ambavyo vimesababisha vifo vya mamia kwa maelfu ya watu na kuwalazimisha wengine milioni 1.7 kukimbilia katika makambi.

Serikali ya Uganda inawashutumu waasi hao kwa kuvunja makubaliano , kutokana na kushindwa kwao kujikusanya katika makambi. Kamanda wa jeshi la Uganda Luteni Jenerali Arouda Nyakairiwa amewaonya hata hivyo wapiganaji hao kutoacha mazungumzo ya Juba.

Waasi wa LRA wamekiri kuvunja makubaliano hayo na pia wameionya serikali ya Marekani kutowapiga vita.

Akihojiwa na gazeti la Daily Monitor la Uganda naibu kamanda wa LRA Vincent Otti amekiri kuwa wapiganaji wake hawakujikusanya katika maeneo wanayotakiwa kujikusanya kutokana na kuzingirwa na jeshi la Uganda,na hivyo kuishutumu serikali kuwa ndio inavunja makubaliano.