1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hali Inatisha Katika Jamhuri ya Afrika Kati

24 Desemba 2013

Ufaransa imeelezea msimamo wake wa kutoelemea upande wowote katika mzozo wa Jamhuri ya Afrika kati,msimamo ambao wataalam wanahisi ni shida kuutekeleza katika wakati ambapo mshirika wake wa karibu Chad,haiufuati.

https://p.dw.com/p/1AgGz
Maandamano ya wafuasi wa opereshini ya Ufaransa Sangaris katika Jamhuri ya Afrika katiPicha: MIGUEL MEDINA/AFP/Getty Images

Mjini Bangui,wanajeshi wa Tchad wanaotumikia kikosi cha kulinda amani cha Umoja wa Afrika wamewafyetulia risasi waandamanaji waliokuwa wakiwataka warejee makeao kwa tuhuma za kuwa karibu zaidi na waasi wa Seleka walionyakua madaraka mwezi Machi mwaka huu nchini humo.Mwanaharakati mmoja ameuwawa.

Serikali ya Chad imekanusha kuhusika na mashambulio hayo.

Mashambulio yameripotiwa pia kati ya wanajeshi wa Chad na wale wa Burundi wanaotumikia kikosi cha MISCA. Wanajeshi wa Chad wanasemekana waliwarushia guruneti wanajeshi wa Burundi walipokuwa wakiwapokonya silaha waasi wa zamani wa Seleka.

"Wanajeshi wa Chad wameondoka pamoja na waasi wote sita wa Seleka na kuanza kufyetua risasi kila upande,wamerejea baadae na kuanza kushambulia vituo vyetu" mkuu wa kikosi cha Burundi Luteni kanali Pontien Hakizimana amesema.

Ufaransa Yasema Haielemei Upande Wowote

Duru za kijeshi zinasema uhusiano kati ya wanajeshi wa Chad na wale wa Burundi katika kikosi cha MISCA,umezorota tangu wanajeshi wa Chad walipowekwa nje ya mji mkuu na wanajeshi wa Burundi kupewa jukumu la kulinda amani mjini Bangui.

Französische Truppen patrouillieren in Zentralafrikanischer Republik 7.12.13
Wanajeshi wa Ufaransa wanapiga doria mjini BanguiPicha: Reuters/Emmanuel Braun

Ikionyesha hamu ya kutaka kuendelea kuwa na mshirika wake katika eneo hilo,anayewasaidia pia katika vita dhidi ya ugaidi nchini Mali,Ufaransa imeelezea umuhimu wa kujulikana ukweli kuhusu kuuliwa mwanaharakati huyo.Ufaransa imeelezea pia "imani yake kamili kwa rais Idriss Deby wa Chad,mshirika mkubwa aliyetuma wanajeshi 850 katika kikosi cha kulinda amani cha MISCA katika Jamhuri ya Afrika kati.

Katika wakati ambapo wanajeshi wa Ufaransa wanalaumiwa na waandamanaji wanaowaunga mkono Seleka kufanya mapendeleo rais Francois Hollande amesisitiza kuhusu misingi ya kutoelemea upande wowote wanajeshi wa Ufaransa.

Maandamano dhidi ya Opereshini Sangaris

Licha ya ahadi hizo maandamano yameripoitiwa tena dhidi ya opereshini za wanajeshi wa Ufaransa Sangaris katika Jamhuri ya Afrika Kati.

Ahmet Adam vor der Moschee
Ahmed Adam akisimama mbele ya msikiti mjini BanguiPicha: DW/S. Schlindwein

"Tunapinga ukoloni wa Ufaransa,hatuitaki Ufaransa na hatuitaki opereshini Sangaris" ni miongoni mwa madai ya waandamanaji huku wengine wakisema "hawataki vita vya kidini katika nchi yao."

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/AFP

Mhariri. Mohammed Abdul-Rahman