1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

HARARE:Zimbabwe yasema Brown anapoteza muda wake kutishia kususia mkutano

20 Septemba 2007
https://p.dw.com/p/CBO8

Zimbabwe imesema kuwa Waziri Mkuu wa Uingereza Gordon Brown anapoteza muda wake kwa kutoa tishio la kususia mkutano wa kilele wa viongozi wa Ulaya na Afrika iwapo Rais Mugabe ataalikwa.

Naibu Waziri wa Habari wa nchi hiyo Bright Matonga amesema kuwa Rais Mugabe amealikwa kuhudhuria mkutano huo, mjini Lisbon Ureno.

Amesema kuwa Rais Mugabe ataiwakilisha Zimbabwe hata kama Waziri Mkuu huyo wa Uingereza atasusa au la.

Umoja wa Ulaya umemwekea vikwazo vya kusafiri kiongozi huyo wa Zimbabwe mwenye umri wa miaka 83.

Ureno ambayo kwa sasa ndiyo rais wa Umoja wa Ulaya imeelezea nia yake ya kutotaka kumbagua Mugabe katika mkutano huo uliyopangwa kufanyika mwezi Desemba mwaka huu.