1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hatma ya Ukraine kuamuliwa mjini Minsk

Christoph Hasselbach11 Februari 2015

Mji mkuu wa Belarus Minsk utakuwa mahala pa maamuzi muhimu katika mgogoro wa Ukraine Jumatano hii. Rais Alexander Lukashenko anaonekana kama mtu asiegemea upande, lakini mara nyingi muonekano hudanganya pia.

https://p.dw.com/p/1EZNe
Minsk Alexander Lukaschenko Wladimir Putin Treffen 10.10.2014
Picha: Reuters/Vasily Fedosenko

Hata mbele ya Berlin, mji wa Minsk umekuwa eneo muhimu zaidi kwa juhudi za kidiplomasia katika mgogoro wa Ukraine. Mwishoni mwa mwezi Agosti 2014, marais Petro Poroshenko na Vladimir Putin walikutana mjini humo kwa duru ya kwanza ya mazungumzo binafsi. Mwezi Septemba, wawakilishi wa serikali ya Kiev walikutana na viongozi wa waasi wanaowania kujitenga kutoka mashariki mwa Ukraine mjini Minsk, na wakakubaliana juu ya mpango wa mani. Makubaliano hayo yamevunjwa tangu wakati huo. Waasi wanaowania kujitenga wamefanya mashambulizi, na mapigano mashariki mwa Ukraine ni makali mno.

Siyo jambo la bahati kwamba mji wa Minsk umekuwa mahala muhimu kwa majadiliano. Belarus imejidhihirisha kama taifa lisiloegemea upande tangu ulipoanza mgogoro wa Ukraine karibu mwaka mmoja uliyopita. Mwishoni mwa mwezi Februari mwaka 2014, muda mfupi kabla ya Urusi haijaiteka rasi ya Crimea, Lukashenko alizungumzia juu ya kuheshimu uhuru wa mipaka ya Ukraine. Tofauti ya Urusi, aliitambua mara moja serikali mpya ya Ukraine, na mwezi Mei Lukashenko alimpongeza rais mpya Petro Poroshenko kufuatia ushindi wake - na alialikwa kwenye hafla ya kuapishwa kwa rais huyo mjini Kiev. Aliitembelea Kiev kwa mara nyingine mwishoni mwa Desemba 2014, kufanya majadiliano na Poroshenko.

Rais wa Belarus Alexander Lukashenko.
Rais wa Belarus Alexander Lukashenko.Picha: DW/E. Daneiko

Kutoegemea upande kwa uongo

Katika hali halisi hata hivyo, Lukashenko ni mshirika wa muda mrefu wa Urusi. Watu wachaceh watakumbuka kuwa mwaka 1997, Urusi na Belarus walianzisha taifa la pamoja linaloendelea kuwepo rasmi hadi hii leo. Belarus na Urusi pia wanachama waanzilishi wa muunagno wa kiuchumi wa Eurasian. Mkataba wa muungano huo ulinza kutekelezwa Januari 1, mwaka huu wa 2015. Wakati mataifa hayo mawili yanatofautiana mara kwa mara kuhusu masuala ya kibiashara, Moscow na Minsk zinaheshimu usihirika wao.

Mataifa hayo mawili pia yanashirikiana kwa karibu katika sekta ya kijeshi. Yote ni wanachama wa shirika linalodhibitiwa na Urusi la "Collective Security Treaty." Urusi inaendesha vituo vya rada na imeweka ndege zake za kivita na helikopta nchini Belarus. Na kufikia mwaka 2016, Urusi inataka kujenga kituo cha jeshi la anga katika mji wa Belarus wa Bobruisk, karibu kilomita 250 kaskazini mwa mpaka wa Ukraine.

Msaada, na siyo upatanishi

Urafiki wa hivi karibuni kati ya Belarusi na Ukraine ni tukio jipya kwa mujibu wa Astrid Sahm, mtalaamu wa Belarus na mtafiti wa nje katika kituo cha masuala ya kimataifa na usalama cha mjini Berlin SWP. "Licha ya kukataa kwake kile kilichojulikana kama mapinduzi ya rangi, Lukashenko tayari alikuwa na mawasiliano mazuri na rais wa wakati huo, Viktor Yuschenko, baada ya mwaka 2014, Astrid aliiambia DW, na kuongeza kuwa hiyo ndiyo sababu Ukraine ilimuomba Lukashenko msaada baada ya kubadilika kwa utawala mjini Kiev.

Lukashenko anasema anapendelea kutoa msaada kuliko upatanishi. "Sisi siyo wapatanishi, na hatukuliomba jukumu hilo," alisema katika mkutano na waandishi wa habari mwishoni mwa mwezi Januari. Urusi inaendelea kuwa kimya juu ya njia ya urafiki anayoichukuwa Lukashenko kuelekea watawala wapya mjini Kiev. Waangalizi wanashuku hii ndiyo njia ya Moscow kubakiza wazi njia za mawasiliano na Kiev. Baadhi ya wanasiasa wa Urusi hata hivyo, wamemtuhumu Lukashenko kwa kusimama upande usiyo sahihi.

Kansela Merkel na rais Francois Hollande walipokutana na rais Putin mjini Moscow.
Kansela Merkel na rais Francois Hollande walipokutana na rais Putin mjini Moscow.Picha: picture-alliance/epa/S. Ilnitsky

Hatimaye "dikteta wa Ulaya aliebakia" akubalika tena

Nje ya nchi, Lukashenko anaonekana kunufaika na huduma zake za kidiplomasia katika mgogoro wa Ukraine. mataifa ya Magharibi yanamtizama rais huyo wa Belarus kama "Dikteta wa mwisho barani Ulaya", na Umoja wa Ulaya umemuwekea vikwazo pamoja na wajumbe wengine wa serikali yake. Sasa akiwa kama mwenyeji wa mazungumzo ya amani, ana uwezekano mkubwa wa kushikana mkono na Kansela Angela Merkel wa Ujerumani na rais wa Ufaransa Francois Hollande.

Na siyo hilo tu. Latvia, ambayo kwa sasa inashikilia urais wa mzunguko wa Umoja wa Ulaya, haiondowi uwezekano wa kumualika Lukashenko katika mkutano wa ushirkiano kati ya Umoja wa Ulaya na mataifa ya Ulaya Mashariki utakaofanyika mwezi Mei mjini Rigan. Hajakaribishwa katika mikutano ya wakuu wa mataifa na serikali za Umoja wa ulaya mpaka sasa.

Mwaliko kwenda mjini Riga utampatia Lukashenko point, pamoja na raia wa Belarus. Uchaguzi wa rais umepangwa kufanyika Septemba mwaka huu wa 2015, na rais huyo ambaye amekaa madarakani tangu mwaka 1994, anapanga kugombea nafasi hiyo kwa mara nyingine.

Mwandishi: Goncharenko Roman
Tafsiri: Iddi Ssessanga
Mhariri: Elizabeth Shoo