1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Havertz aondoka kambini kuelekea Chelsea

Deo Kaji Makomba
4 Septemba 2020

Mshambuliaji wa kimataifa wa Ujerumani Kai Havertz ameondoka katika kambi ya mazoezi ya timu ya taifa ya Ujerumani Ijumaa (04.09.2020) kwenda kujaribu kukamilisha uhamisho wake kuelekea klabu ya Chelsea ya England

https://p.dw.com/p/3i16C
Uefa Europa League Inter Mailand vs Leverkusen
Kai Havertz mwenye jezi nyekundu namba 29 akiwajibika kaziniPicha: Getty Images/AFP/M. Meissner

Mkurugenzi wa spoti wa klabu ya Leverkusen Rudi Voeller, alisema Havertz anasafiri kwenda London "ili Kai sasa aweze kutatua mambo huko London kwa msaada wetu."  

Kocha mkuu wa timu ya taifa ya Ujerumani Joachim Loew, alisema anatarajia Havertz atasaini mkataba wa kuichezea klabu ya Chelsea hivi karibuni.

"Tulijua kwamba sasa, leo au kesho maelezo ya mwisho yalikuwa yanamanisha kutatuliwa katika mkataba wake na Chelsea,"alisema Loew katika vidio iliyochapishwa kwenye wavuti ya Shirikisho la soka la Ujerumani, akiongeza kuwa Havertz"hakika anataka kuchukua hatua hii."

Havertz alikuwa mchezaji wa akiba ambaye hakutumiwa wakati wa mechi ya Ujerumani na Uhispania Alhamisi kwenye Ligi ya Mataifa na kutoka sare ya 1-1. Low alisema alikuwa anafahamu endapo Havertz angecheza na kuumia katika mchezo huo ingeweza kuhatarisha mchakato wake wa uhamisho kuelekea Chelsea.

Kusainiwa kwa Havertz kunaweza kukamilisha ukarabati wa kikosi cha Chelsea ambayo pia imeshuhudia mshambuliaji nyota wa Ujerumani Timo Werner, winga Hakim Ziyech, beki wa kati Thiago Silva na beki wa kushoto Ben Chilwell wakisogea kwenda katika Klabu hiyo ya England.

"Tunafahamu umuhimu wa hili kwa Bayer 04 Leverkusen na Kai na nataka kuliangalia suala hili  kiuwajibikaji, alisema Oliver Bierhoff meneja wa timu ya taifa ya Ujerumani. "Wakati huo huo ni heshima na tofauti kwa soka la Ujerumani wakati wachezaji chipukizi wa Ujerumani wanahitajika katika vilabu bora vya soka vya kimataifa."

Havertz kwa mara ya mwisho aliichezea Leverkusen katika robo fainali ya michuano ya Ligi ya Europa manamo Agosti 10, akifunga bao katika mechi waliopoteza 2-1 dhidi ya Inter Milan.

Kocha wa Leverkusen Peter Bosz amesema hatarajii kumuona Havertz katika kikosi chake kwa msimu mpya wa Bundesliga.

Chanzo/APE