1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hisia za Waghana na Wakenya kuhusu ziara ya Obama

Akwiri Joseph10 Julai 2009

Wakenya walalamika Waghana washangilia

https://p.dw.com/p/IlGi
Mfanyabiashara akiuza shati za picha ya rais Barack Obama katikati mwa AccraPicha: AP

Rais wa Marekani Barrack Obama alifanya uamuzi kuzuru taifa la Ghana katika ziara yake ya kwanza barani Afrika tangu alipochukua wadhifa wa rais wa Marekani mapema mwaka huu.

Hatua hii imewaghadhabisha raia wengi nchini Kenya ambao walimtarajia Obama kuzuru Kenya kwanza, taifa ambalo anatoka babake mzazi.

Raia wengine nchini humo wamesema hatua ya Obama kutozuru Kenya ni kwa sababu ya kutoridhishwa kwake na jinsi serikali ya muungano nchini humo inavyoendesha shughuli zake.

Raia hawa wametaja hatua hiyo kama ujumbe unaonuiwa kuwasukuma viongozi nchini humo kubadilisha sera zao za uongozi na kuimarisha utenda kazi wao.

Na wakenya wakiendelea kutafakari hatua ya rais huyo wa Marekani, nchini Ghana ziara ya Obama imesubiriwa kwa hamu kuu, huku wengi wa raia waliofurahia hatua hiyo wakiitaja kama baraka kwa taifa hilo.

Kulingana na wengine ziara hiyo inadhihirisha jinsi taifa hilo linavyothaminiwa na jamii ya kimataifa.

Akieleza sababu ya kutozuru Kenya, Obama alisema alikuwa tayari amezuru nchi hiyo wakati akiwa seneta wa jimbo la Ilinois huko Marekani na kwamba hakutaka kuonekana kama anayependelea nchini yoyote.

Taarifa za awali kutoka ikulu ya Whitehouse zilisema kwamba Obama aliazimia kuimarisha uhusiano wa Marekani na Ghana, na kusistiza umuhimu wa demokrasia na uongozi bora katika kufanikisha maendeleo ya taifa hilo.

Licha ya matarajio makubwa ya bara la Afrika kutoka kwa kuchaguliwa kwa Obama kama rais wa Marekani, bara hilo maskini halijapewa kipaumbele na rais Obama ambaye amezingatia zaidi vita nchini Iraq na Afghanistan, na misimamo ya kinuclear ya Iran na Korea Kaskazini.

Ziara ya Obama nchini Ghana si ya kwanza kwa rais wa Marekani, huku marais wa awali Bill Clinton na George Bush wakiwa walizuru taifa hilo wakati wa hatamu zao za uongozi.

Akieleza sababu ya kutozuru Kenya, Obama alisema alikuwa tayari amezuru nchi hiyo wakati akiwa seneta wa jimbo la Ilinois na kwamba hakutaka kuonekana kama anayependelea nchini yoyote.

Na ziara ya Obama nchini Ghana si ya kwanza kwa rais Marekani, huku marais wa awali Bill Clinton na George Bush wakiwa walizuru taifa hilo wakati wa hatamu zao za uongozi.

Mwandishi:Joseph Akwiri

Mhariri: Miraji, Othman