1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hofu yazidi kuhusu Urusi kujitowa katika mkataba wa INF

Saumu Mwasimba
5 Julai 2019

Urusi inailaumu Marekani kwamba imejitowa kwenye makubaliano ya kusitisha matimizi ya makombora ya nyuklia ya masafa marefu uliofikiwa enzi za vita baridi

https://p.dw.com/p/3Lesa
Brüssel Jens Stoltenberg, NATO-Generalsekretär
Picha: picture-alliance/Anadolu Agency/D. Aydemir

Jumuiya kujihami ya NATO inasema hakuna dalili ya Urusi kusalimu amri katika mgogoro wa makombora. Mkuu wa NATO Jens Stoltenberg ameonya kwamba nafasi ya kuukoa mkataba  kuhusu silahauliofikiwa wakati wa vita baridi inapungua kila siku.

Kauli ya Stoltenberg imekuja baada ya kufanyika mazungumzo na maafisa wa Urusi  ambayo yameshindwa kufikia mwafaka wa aina yoyote. Urusi na Marekani zote zilisitisha hatua ya kushiriki kwenye mkataba wa kuondowa makombora ya Nyuklia ya  masafa ya kati  kila mmoja akimtuhumu mwenzie kwamba  amekiuka mkataba huo ambao kimsingi ulipiga marufuku matumizi ya makombora yote ya Nuklia ya uwezo wa kati.

 Marekani hakuna shaka kwamba itajiondowa kwenye mkataba huo mwezi Agosti ikiwa Urusi haitoharibu mfumo wake tata wa makombora ambao Marekani na jumuiya ya NATO zinasema unakiuka makubnaliano yaliyosainiwa mwaka 1987 kati ya rais wa Marekani Ronald Reagan na kiongozi wa Soviet Mikhail Gorbachev.

Russland | Hochwasser in Irkutsk Wladimir Putin
Picha: picture-alliance/dpa/M. Klimentyev

Kutoweka kwa matumaini ya kupatikana mwafaka kumekuja baada ya jumuiya ya Nato kufanya mazungumzo na maafisa waandamizi wa Urusi kama sehemu ya juhudi za kuyaokoa makubaliano hayo wiki moja baada ya mawaziri wa ulinzi wa muungano huo wa kijeshi kukubaliana juu ya mpango wa kuchukua hatua za kujibu mapigo endapo serikali ya mjini Moscow itapuuza muda wa mwisho uliowekwa. Hata hivyo rais Putin akizungumzia msimamo wa nchi yake kuhusu mkataba huo wa enzi za vita baridi aliendelea kuilaumu zaidi Marekani.

''Kama nilivyosema,Marekani imechukua uamuzi wa kivyake na kujiondowa kwenye mkataba wa kupinga matumizi ya makombora ya kasi kubwa na hivi karibuni inaondoka kwenye makubaliano ya INF pia.Lakini mara hii haikujiondowa tu lakini imetafuta sababu ya kuondoka kwa sababu hili ni jukwaa la vita,jukwaa la vita katika Ulaya huenda lisiwe na ya kufurahisha kwa marekani licha ya kutanuka kwa NATO na kupelekwa kikosi cha Nato karibu na mipaka yetu.''

Katika jumuiya ya NATO Stoltenberg amekataa kutowa maelezo zaidi ya hatua zitakazofuata kuelekea Urusi hii leo akisema jumuiya hiyo bado inaelekeza zaidi juhudi za kujaribu kuunusuru mkataba huo wa INF ingawa pia amesema mfumo wa ulinzi wa makombora ya masafa marefu  ya muungano huo uliopo hivi sasa hauwezi kuwa na uwezo wa kuyaangusha makombora ya Urusi.Mabalozi wa nchi za Nato leo watakutana na wenzao wa urusi kujaribu juhudi za mwisho za kuishawishi nchi hiyo izingatie mkataba huo wa kuachana na silaha za Nyuklia uliotiwa saini mwaka 1987.

Mwandishi: Saumu Mwasimba

Mhariri Josephat Charo