1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Homa ya nguruwe inazidi kusambaa

Munira Mohammad29 Aprili 2009

Maafisa nchini Ujerumani wamethibitisha visa vitatu vya homa ya nguruwe nchini ujerumani.

https://p.dw.com/p/HgNd
Virusi vinavyosababisha homa ya nguruwe vimegunduliwa Ujerumani.Picha: AP


Mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 22 kutoka Hamburg, mwanamume mmoja kutoka mji wa Ragensburg na mwanamke mmoja kutoka mkoa wa Bavaria ndio imethibitishwa wameambukizwa homa hii ya nguruwe. Maafisa wa afya nchini Ujerumani wanasema bado pia wanachunguza visa vingine kuthibitisha kama ni homa hii ya nguruwe. Visa vinne vimeripotiwa katika nchi mbili za ulaya, visa viwili Uingereza na viwili Uhispania. Lakini hadi sasa ni nchini Mexico tu ndio imeripotiwa vifo - watu 159 wamefariki.


Homa ya nguruwe ambayo kwanza iligunduliwa nchini Mexico, inaendelea kusambaa duniani. Hapa nchini Ujerumani maafisa wa afya wamethibitisha visa vitatu vya homa hii ya nguruwe. Kisa cha kwanza kiliripotiwa hapa Ujerumani ilikuwa ni mtu mmoja aliyekuwa ziarani Mexico, anatoka huko Mallersdorf karibu na mji wa Regensburg.


Mexiko Schweinegrippe Passanten mit Mundschutz
Kufunika uso ni mojawapo ya tahadhari za kuzuia homa ya nguruwe.Picha: picture alliance / landov

Idadi hii hata hivyo sasa imeongezeka, baada ya maafisa wa afya kuchunguza visa vingine sita vya maambukizi haya ya homa hii ya nguruwe- wamethibitisha mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 22 kutoka Hamburg anaugua homa hii ya nguruwe. Kisa kingine kilichothibitishwa hapa Ujerumani ni kutoka mkoa wa Bavaria, mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 37.


Bado maafisa wanaendelea kuchunguza visa vingine kubainisha iwapo ni homa hii ya nguruwe au ni homa tu ya kawaida. Mbali na Ujerumani- ulaya sasa imethibitisha visa saba vya homa hii ya nguruwe- visa viwili viliripotiwa nchini Uingereza, Viwili nchini Uhispania na sasa vitatu Ujerumani. Nchini MAREKANI idadi ya wanaougua homa hii ya nguruwe imeongezeka hadi watu 64, huku wataalam wakisema wanataraji sasa vifo kadhaa vitatokea jinsi homa hii inavyosambaa.


Shirika la afya duniani WHO limesema litaanda mkutano wa wanasayansi kubadilishana mawazo namna homa hii inavyosambaa na vipi watapata tiba. Watalaam wa afya kutoka Marekani na Mexico, chanzo cha homa hii ya nguruwe.


Mexico ndio nchi pekee imeripoti vifo- idadi hadi kufikia sasa ni 150 huku watu wengine 1,600 wakithibitishwa wanaugua homa hii ya nguruwe. Kaimu Mkurugenzi wa usalama wa afya wa shirika la afya duniani WHO Keiji Fukuda anasema hadi sasa haijabainika ni kwa nini virusi vya homa hii nchini Mexico vina makali sana kuliko maeneo mengine .


Watalaam kutoka Marekani na Mexico watashiriki katika mkutano huu uliotishwa na shirika la afya duniani, na baadaye WHO imesema itatoa ripoti yake baadaye hii leo.


Kwingine duniani, watu wanaendelea na tahadhari huku wasafiri wakipimwa katika viwanja vya ndege ili kuzuia kusambaa kwa homa hii ya nguruwe.


Mwandishi: Munira Muhammad/ reuters, afpe

Mhariri: Abdulrahman