1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Homa ya nguruwe yahanikiza

Oumilkher Hamidou28 Aprili 2009

Kiwewe hakisaidii kitu wanaonya wataalam

https://p.dw.com/p/Hfgf
Wapita njiani na kinga ya homa ya nguruwePicha: picture alliance / landov

Kuachishwa kazi kocha wa timu ya Bayern Munich Klinsmann na mjadala kuhusu kiwango cha siku za mbele cha malipo ya uzeeni ndizo mada zilizochambuliwa zaidi na wahariri wa magazeti ya Ujerumani hii leo.Lakini kwanza wamejishughulisha na homa ya nguruwe.Na gazeti la DIE WELT linaandika:

Baada ya kuihama nchi yao ya asili na kuingia Marekani,hiivi sasa wameshaingia Ulaya na pengine wameshafika Ujerumani.Jee virusi hivyo vya aina mpya vinavyokiuka bahari vimechukua sura mpya?Kwanza tunabidi tuseme hilo si jambo la ajabu.Kila wakati ambapo maradhi yatakua yanaenezwa na watu wanaotembela nchi moja hadi nyengine,itafika wakati tuu yatatoka bara moja na kuingia katika jengine.Kwa mujibu wa maelezo yaliyotolewa,hakuna bado barani Ulaya kisa cha mtu aliyeambukizwa homa ya nguruwe na binaadam mwenzake.Hakuna kwa hivyo haja ya kuingiwa na wasi wasi,wanasema wataalam.Lakini nasaha yao haisaidii kitu kwasababu hofu na wasi wasi vimeshazagaa."

"Hatari isiyokadirika" ndio kichwa cha maneno cha ripoti ya gazeti la SÜDDEUTSCHE ZEITUNG linaloandika:

Kufumba na kufumbua watu wanazungumzia juu ya maradhi ya kuambukiza yanayotishia kuenea kote ulimwenguni.Picha za watu waliofunga vitambaa katika sehemu ya puwa na mdomo,shule zilizofungwa na vituo vya maonyesho,zinabainisha wazi kabisa kwamba hofu zimezagaa hata kabla ya virusi kuenea.Chanzo chake ni maradhi hayo ya kuambukiza.Kwasababu kama vile virusi vinavyotapakaa haraka ndivyo nazo ripoti zinavyoenea kwa kasi katika kila pembe ya dunia-na kuna ripoti za kuaminika sawa na nyenginezo ambazo ni za kuchochea kiwewe.Inawezekana kuiona homa ya nguruwe ikitoweka muda mfupi tuu kutoka sasa.Hakuna mtaalam yeyote anaeweza kuashiria janga hili litakua la aina gani.Pengine likagharimu maisha ya watu wa mabara yote na kuonyesha jinsi ulimwengu uliogeuka kua pua na mdomo unavyoweza kuathirika licha ya maendeleo yote ya kitabibu yaliyoko."

Gazeti la SÄCHSISCHE ZEITUNG linazungumzia kauli ya waziri wa ajira na huduma za jamii Olaf Scholz aliyesema malipo ya uzeeni hayatapunguzwa mwakani.Gazeti linaendelea kuandika:

"Hakuna serikali yoyote itakayosubutu kuwatumia watu milioni 20 wanaolipwa pensheni, kua mada ya kupigiwa upatu katika kampeni ya uchaguzi.Kile ambacho Scholz hajakifichua lakini ni jee malipo ya uzeeni yatapatikanaje ikiwa fedha wanazochangia waajiriwa katika bima ya jamii,zitakua haba kuliko ilivyotarajiwa?Ndio maana malipo ya uzeeni haya uhakika-kinyume na asemavyo Olaf Scholz.

Gazeti la WESTDEUTSCHE ALLGEMEINE ZEITUNG ni miongoni mwa magazeti yaliyoandika kuhusu hatima ya kocha wa timu ya Bayern Munich Jürgen Klinsmann.Gazeti linahisi ukosefu wa magoli sio sababu pekee!Gazeti linaendelea:

"Kabumbu ni sawa na ulimwengu wa kihafidhina ambapo kocha anatajikana kua professor eti kwasababu anavaa miwani.Na Klinsmann alikua na ruya.Kansela wa zamani Helmut Schmidt aliwahi kusema,mwenye ruya anabidi ende kwa daktari wa macho.Mfuasi huyo wa imani ya Budhha alikua akivumiliwa kila ushindi unapopatikana.Lakini suala linalojitokeza ni jee,Klinsmann mwenyewe hana hatia?Jibu ni la.Makosa yake yanapindukia kila ripoti ya mchezo."


Mwandishi:Hamidou Oummilkheir

Mhariri:Abdul Rahman