1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Inawezekana ulimwengu bila silaha za Nuklia asema Obama

5 Aprili 2009

Maelfu wajitokeza kusikiliza Hotuba ya Obama mjini Prague

https://p.dw.com/p/HQkA
Rais Obama na mkewe Michelle wakisalimiana na watu baada ya hotuba yake mjini PraguePicha: AP

Rais Barack Obama wa Marekani ametoa hotuba yake ya kwanza kubwa mbele ya hadhara barani Ulaya tangu alipoingia madarakani ambapo ametoa mwito kwa ulimwengu kutia juhudi katika kuondoa silaha za kinuklia pamoja na kuzuia majaribio ya silaha hizo.Rais Obama amesema

"Marekani ikiwa ni nchi pekee yenye nguvu za kinuklia iliyowahi kuzitumia silaha hizo ina jukumu kubwa la kimaadili la kuchukua hatua.Hatuwezi kufanikiwa katika suala hili tukiwa peke yetu lakini tunaweza kuanzisha juhudi hizo.kwahivyo leo nasema wazi na nikiwa na matumaini kwamba,Marekani inajitolea kutafuta mafanikio ya kuwepo amani na usalama katika dunia itakayokua bila ya silaha za kinuklia''

Akizungumza mbele ya umati wa watu kiasi cha 30 elfu katikati ya mji mkuu Prague rais huyo wa Marekani pia amekitaja kitendo cha Korea Kaskazini cha kufanya majaribio ya roketi yake ya masafa marefu kama ni uchokozi ambao haupaswi kupuuzwa.

Amezungumzia pia kuhusu harakati za kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa akisema Marekani iko tayari kuongoza katika makabiliano hayo.Hotuba yake mjini Prague imetajwa kuwa hotuba muhimu kuhusu sera za nje za Marekani katika ziara yake ya siku nane barani Ulaya.Rais Obama kesho atakuwa nchini Uturuki ambako amepangiwa kukutana na viongozi wa nchi hiyo.Tayari kumekuwa na maandamano nchini humo ya kupinga ziara hiyo.Ziara ya Obama Uturuki itakuwa ni ziara yake ya kwanza katika nchi ya kiislamu.

Mwandishi Saumu Mwasimba/ZR