1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Safari ya anga.

Mtullya, Abdu Said22 Oktoba 2008

India imeanza mradi wa miaka miwili katika utafiti wa mwezi.

https://p.dw.com/p/Feh9
Chombo cha anga cha India Chandrayaan.Picha: picture-alliance/dpa

India imefanikiwa kurusha chombo cha anga kisichokuwa na mwanaanga, ikiwa ni hatua ya kwanza muhimu katika mpango wa kuelekea mwezini.Chombo hicho Chandrayaan namba moja, kitafanya safari ya utafiti kwa muda wa miaka miwili.


Safari ya chombo hicho ilianza bila ya dosari kutoka kwenye kituo kilichopo kusini mwa jimbo la Andhra Pradesh. Chombo hicho kitazunguka mwezi ili kutayarisha ramani ya mwezi na kuchunguza sehemu ambapo pana raslimali.

Kuanza kwa safari ya chombo hicho ni hatua muhumi sana kwa India katika juhudi zake kuenda sambamba na nchi zingine za bara la Asia zinazotekeleza miradi ya utafiti wa anga za mbali , China na Japan.

Akisisitiza umuhimu wa hatua hiyo ya kwanza mkurugenzi wa shirika la utafiti wa anga nchini India Madhavan Nair amesema kuanza kwa safari hiyo leo ni wasaa wa kihistoria kwa India

Lengo la mradi huo unaoitwa Chandrayaan, yaani chombo cha mwezi ni kutayarisha ramani ya mwezi katika nyanja tatu-kuonesha,elementi,madini na mahala penye raslimali,. Lengo la mradi huyo pia ni kutafuta akiba za maji katika mwezi.

Chombo cha Chandrayaan kimebeba vifaa 11 vitakavyofanyiwa utafiti.Chombo cha Chandrayaan kinachoendeshwa kwa nishati ya jua kina uzito wa kilogramu 1380.

Chombo hicho kitafanya utafiti wa gesi ya helium inayoaminiwa kuwapo kwa wingi kwenye mwezi. Gesi hiyo ni muhimu katika utafiti wa nyuklia na pia ni muhimu katika uzalishaji wa nishati.

Chombo hicho kinatarajiwa kudondosha bendera ya India tarehe 15 mwezi ujao, kuashiria kwamba India pia ina maslahi kwenye mwezi. Kwa kupeleka chombo hicho angani India imeingia katika kundi la nchi zinazodhibiti tekinolojia ya utafiti wa anga za mbai , ikiwa pamoja na Marekani ,Urusi, na China.

India ilianzisha mradi wa utafiti wa anga za mbali mnamo mwaka 1962 na ilifanikiwa kurusha satelaiti ya kwanza mnamo mwaka 1984. Nchi hiyo pia imetangaza mpango wa kupeleka wanaanga wawili watakaofanya safari ya wiki mbili angani mnamo mwaka 2015.