1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Iran kuipiku Marekani mzozo wa Ghuba

Amina Mjahid
7 Februari 2018

Mvutano unaozidi kati ya Qatar na Umoja wa Falme za Kiarabu juu ya ndege zao za kijeshi unatishia maslahi ya kimkakati ya Marekani katika eneo la Guba na huenda hali hiyo ikainufaisha adui wa eneo hilo Iran.

https://p.dw.com/p/2sDur
Ägypten Außenminister Treffen in Kairo
Picha: Reuters/K. Elfiqi

Abu dhabi inasema ndege za kijeshi za Qatar  zilizuwiya ndege mbili za abiria za Umoja wa Falme za kiarabu zilipokuwa zinaelekea Bahrain mwezi uliyopita, huku Doha nayo ikisema ndege za kijeshi za umoja wa falme za kiarabu ziliingia bila ruhusa katika anga yake mnamo Desemba tarehe 21 na Januari tarehe tatu.

Kila upande unakanusha shutuma za mwingine, na nchi hizo mbili ambazo zote zinazalisha nishati zinajaribu kutuliza mgogoro huo. Hatari ya makabiliano kati yao imeongezeka lakini uwezekano wa kuzuka mapigano kati ya nchi hizo mbili haupo, hii ikiwa ni kulingana na wataalamu katika eneo hilo.

Kuongezeka kwa mvutano miezi saba baada ya Umoja wa falme za kiarabu, Saudi Arabia, Bahrain na Misri kuiwekea Qatar vikwazo vya usafiri na biashara kwa Qatar kufuatia madai iliyoyakanusha kwamba inaunga mkono ugaidi na kumuunga mkono adui wa eneo hilo ambaye ni Iran, kumeishitua  Marekani.

"Inapotokea ndege za kijeshi za Qatar kupishana kwa karibu na ndege za abiria, ipo hatari ya kutokea tukio ambalo hata kama halikupangiwa linaweza kusababisha maisha ya watu kupotea na kupanua suala hili kuwa jambo ambalo nchi za Guba hazijawahi kuliona miongoni mwao ," alisema mwanadiplomasia mmoja wa Magharibi akizungumza kwa kutotaka kujulikana.

Hali mbaya inaweza kusababisha moto mkubwa

Gabriel Collins,  mtaalamu wa vikwazo vya kifedha katika chuo kikuu cha Rice mjini Texas  Marekani amesema uwepo wa jeshi katika eneo la mgogoro kwa sababu ya vikwazo vya kidiplomasia na kibiashara ni kosa. Amesema cheche ndogo katika hali mbaya inaweza kusababisha moto mkubwa.

Kuwait Arabische Liga 2014
Viongozi wa Umoja wa nchi za Kiarabu walipokutana kujadili mzozo wa GhubaPicha: picture alliance/dpa/Raed Qutena

Kwa upande wake Waziri wa Ulinzi wa Marekani James Mattis amesema kuharibika kwa mahusiano miongoni mwa washirika wake wa Guba kunatatiza mapambano ya marekani dhidi ya wanamgambo wa dola la kiislamu na kudhibiti ushawishi mbaya wa Iran. Hata hivyo Iran imekosoa vikwazo ilivyowekewa Qatar na kutoa wito wa mvutano uliyopo kutatuliwa kwa njia ya mazungumzo. Waziri wa mambo ya kigeni Mohammad Javad Zarif amezungumzia kile alichokisema ni kukosekana mazungumzo katika eneo hilo.

Eneo la Guba ni eneo muhimu la kimkakati kwa Marekani. Kambi ya kijeshi ya tano ya Marekani iko nchini Bahrain na kambi nyengine ya jeshi la angani ya Marekani ya Al Udeid iliyoko Qatar  ni kitovu cha operesheni zake za angani dhidi ya kundi la wanamgambo wa dola la kiislamu.

"Marekani inazichukulia wote Qatar na Umoja wa Falme za kiarabu kuwa washirika muhimu wa eneo la Guba,"alisema msemaji wa jeshi la angani la Marekani huko Qatar, alipokuwa anajibu swali kutoka kwa shirika la habari la Reuters alipotakiwa kutoa maoni yake juu ya suala hilo la mvutano kati ya Qatar na Umoja wa Falme za kiarabu.

Kambi hiyo ya Qatar ni muhimu iwapo Marekani ingelitaka kwenda vitani na Iran ambayo inaishutumu kwa kufadhili ugaidi na ni kitisho kwa uthabiti na maslahi ya Marekani Mashariki ya Kati. Hata hivyo Iran imeendelea kukanusha madai hayo.

Mwandishi: Amina Abubakar/Reuters

Mhariri: Iddi Ssessanga