1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Iran yatangaza maombolezo ya kitaifa

9 Januari 2017

Serikali ya Iran imetangaza siku tatu za maombolezo ya kitaifa kufuatia kifo cha rais wa zamani wa nchi hiyo Akbar Hashemi Rafsanjani, ambaye amefariki baada ya kupata maradhi ya mshtuko wa moyo.

https://p.dw.com/p/2VVTS
Iran Tod von Akbar Hashemi Rafsanjani
Picha: jamaran

Rais Hassan Rouhani akiwa pamoja na viongozi kadhaa wa serikali yake wamefika katika msikiti ulio kusini mwa mji wa Tehran ulikohifadhiwa mwili wa raisi huyo wa zamani. Wakaazi wa mji mkuu wa Iran pia wameelezea majonzi yao kufuatia kifo cha kiongozi huyo ambaye amefariki akiwa na umri wa miaka 82.

Viongozi mbalimbali duniani pia wametuma salam za rambirambi kufuatia kifo cha kiongozi huyo, waziri wa mambo ya nje wa  Bahrain nchi ambayo kwa muda mrefui imeishutumu Iran kuingilia masuala yake ya ndani, ameandika katika ukurasa wake wa twitter kwa kusema "Mungu mbariki Rafsanjani".

Mfalme Hamad bin Isa Al Khalifa amesema kuwa "Ninaomba kwa Mungu roho yake ipumzike kwa amani" huku akimtia moyo rais Iran, raia pamoja na familia ya marehemu.

Mmoja kati ya watoto wa kiume wa Rafsanjan aliyefahamika kwa jina la Yasser amemuelezea baba yake kwa kusema kuwa "alikuwa ni mtu ambaye anafikiria sana kuhusu watu, namaanisha katika kipindi chote ambacho tumekuwa naye, muda wote amekuwa akiwafikiria watu na watu wamekuwa wema sana kwetu, sasa hivi nina hisia za kutokuamini"

Iran Tod von Akbar Hashemi Rafsanjani
Baadhi ya raia wakiomboleza kifo cha RafsanjaniPicha: jamaran

Maryam Rajavi, kiongozi wa tawi dogo la kisiasa la kundi la upinzani la Iran, kundi ambalo kwa kifupi linafahamika kama MEK , kundi ambalo pia wizara ya mambo ya nchi za nje ya Marekani inaliita kuwa ni kundi la kigaidi Mujahedeen e Khalq, katika taarifa yake kiongozi huyo amesema, anaamini kuwa Jamhuri hiyo ya Kiislam itaanguka kufuaatia kifo cha kiongozi huyo.

Saudi Arabia nchi ambayo ina wakaazi wengi wa madhehebu ya Sunni ambayo pia ni mpinzani mkubwa wa kikanda wa Iran yenye washia wengi, haikuweza kutuma mara moja salam za rambirambi, huku moja kati ya televisheni ya taifa ya nchi hiyo ikionyesha mahojiano iliyofanya na kiongozi wa MEK ambayo yanamhusisha Rafsanjani na uteketezaji wa maelfu ya wafungwa mwaka 1988.

Kiongozi wa Kuwait Sheikh Sabah Al Sabah ametuma salamu za rambirambi na kusema "Ninaomba kwa mungu mkuu Allah kumjalia baraka marehemu". Nchi ndogo ya Qatar yenye mipaka ya pamoja ya machimbo ya gesi na Iran imetuma salam zake za rambirambi kupitia kwa mfalme sheikh Tamim bin Hamad Al Than.

Rafsanjan alikuwa rais wa Iran kati ya mwaka 1989 na 1997 kipindi ambacho kilikuwa ni cha mabadiliko makubwa kwa nchi hiyo, hivi sasa nchi hiyo inajitahidi kujenga upya uchumi wa nchi hiyo baada ya vita yake na Iraq mwaka 1980.

Mwandishi: Celina Mwakabwale/AP

Mhariri:Yusuf Saumu