1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Iran yawaachia huru wanamaji wa Marekani

Admin.WagnerD13 Januari 2016

Waziri wa mambo ya kigeni wa Marekani John Kerry ameishukuru Iran leo(13.01.2016) kwa kutatua mzozo kuhusiana na wanamaji 10 wa jeshi la majini la Marekani waliokamatwa , kwa njia ya amani na ufanisi mkubwa.

https://p.dw.com/p/1HcZ0
Iran stoppt zwei Boote der US-Marine
Boti ya doria ya Marekani katika eneo la ghubaPicha: Reuters/U.S. Navy/P. Lewis

Tukio hilo lilianza kwa wanajeshi wa jeshi la majini, tisa wakiwa wanaume na mmoja mwanamke , walipokamatwa baada ya boti mbili za doria kuingia katika mipaka ya Iran jana Jumanne.

"Nataka kueleza shukurani zangu kwa maafisa wa Iran kwa ushirikiano wao katika kulitatua suala hili kwa haraka," Kerry amesema katika taarifa.

Iran stoppt zwei Boote der US-Marine
Wanamaji wa Marekani katika eneo la ghubaPicha: picture-alliance/dpa/US Navy/NMCS/M.L. Turner

"Kwamba suala hili lilitatuliwa kwa amani na uhodari mkubwa ni ushahidi wa uwezo wa kufanyakazi kwa diploamasia katika kuiweka nchi yetu salama, na imara, " Kerry ameongeza.

Iran leo(13.01.2016) iliwaachia wanajeshi 10 wa jeshi la majini kutoka Marekani ambao iliwakamata katika eneo la ghuba, na kuchumua muda wa masaa machache na kuepusha uwezekano wa mzozo wakati ikijitayarisha na kuondolewa vikwazo ilivyowekewa na mataifa ya magharibi.

Watuliza mzozo

Maafisa wa Iran na Marekani walifanya haraka kutuliza mzozo huo , ambao ulijitokeza wakati Iran inajitayarisha hatimaye kukamilisha utekelezaji wa makubaliano ya kinyuklia na mataifa makubwa duniani yenye lengo la kumaliza hali ya muda mrefu ya taifa hilo la jamhuri ya Kiislamu kutengwa kimataifa.

Baada ya mazungumzo yasiyo rasmi kati ya Iran na Marekani , taarifa kutoka jeshi la mapinduzi la Iran , ikielezea wanamaji hao kama wanajeshi wa jeshi la majini la Marekani , ilisomwa katika televisheni ya taifa ikithibitisha kuachiwa kwao.

"Baada ya uchunguzi wa kiufundi na kiutendaji uliofanywa na wanasiasa mahiri na mamlaka ya usalama wa taifa imefahamika kwamba kuingia kwa boti za kijeshi za Marekani katika mipaka ya jamhuri ya Kiislamu ya Iran hakukukusudiwa na kufuatia kuomba msamaha, uamuzi ulichukuliwa kuwaacha huru."

Symbolbild zur Meldung - Iranische Marine gibt Warnschüsse auf Öltanker ab
Maboti ya doria ya Iran yalifyatua risasi za tahadhari dhidi ya meli ya MarekaniPicha: Getty Images/Afp/Atta Kenare

Picha zilizotumika katika ripoti hiyo zimeonesha wanajeshi hao wakiwa wameketi wakiwa watulivu katika mazulia. Iran imesema hapo kabla kwamba wanahudumiwa vizuri. Hakuna ishara kwamba wanajeshi hao walidhuriwa wakati walipokamatwa," taarifa hiyo imesema, na kuongeza kuwa "Jeshi la majini litachunguza mazingira yaliyosababisha wanajeshi hao kuingia Iran."

Vyombo vya mawasiliano viliharibika

Admirali Ali Fadavi , kamanda wa kikosi cha majini cha jeshi la mapinduzi nchini Iran, amesema uchunguzi umegundua kwamba " kuingia huko katika mipaka ya Iran hakukuwa na madhumuni ya uhasama ama nia ya ujasusi" na kwamba wanajeshi hao waliingia katika mipaka ya Iran,"kutokana na kuharibika kwa mfumo wa kuielekeza meli ama boti".

Maafisa wa Marekani walisema moja ama boti zote zilipata matatizo ya kiufundi na zimesukumwa hadi katika kisiwa cha Farsi, ambacho kiko karibu katikati ya Iran na Saudi Arabia. Mawasiliano ya radio yalikatika , ambapo maboti hayo yalikuwa njiani kutoka Kuwait kwenda Bahrain.

Marekani na Iran hazina uhusiano wa kidiplomasia lakini waziri wa mambo ya kigeni wa Marekani John Kerry alimpigia simu mwenzake waziri wa mambo ya kigeni wa Iran Mohammad Javad Zarif kujadiliana kuhusu suala hilo.

Tukio hilo katika eneo la Ghuba limekuja hata hivyo wakati rais Barack Obama akitoa hotuba yake ya mwisho ya hali ya taifa hilo, ikibinya juhudi zozote za kuonesha uhusiano wa karibu na Iran kama sehemu ya kile anachokiacha baada ya utawala wake.

Mwandishi: Sekione Kitojo / afpe

Mhariri: Iddi Ssessanga