1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

ISLAMABAD : Wapinga kuondolewa hakimu mkuu

17 Machi 2007
https://p.dw.com/p/CCIK

Polisi wa kutuliza ghasia nchini Pakistan wamefyetuwa risasi za raba na mabomu ya kutowa machozi kwa waandamanaji na kuwakamata madarzeni ya watu waliokuwa wakipinga kutimuliwa kwa hakimu mkuu wa nchi hiyo.

Polisi pia ilivunja vifaa vya kituo cha televisheni cha binafsi ambacho kilikuwa kikirusha matangazo ya ghasia hizo. Kuvunjwa kwa maandamano hayo kumekuja wakati Hakimu Mkuu wa Mahkama Kuu nchini Pakistan Iftikhar Mohamed Chaudhry alikuwa akisikiliza madai dhidi yake katika baraza la mahkama.

Rais Pervez Musharraf aliamuru kusitishwa kazi kwa hakimu huyo mkuu wiki iliopita kwa kumshutumu kutumia vibaya madaraka yake.Chaudhry anajulikana kuwa mtu wa kujitegemea na amekuwa akiipa changamoto serikali katika kesi kadhaa.

Wale wanaomkosoa Musharraf wanamshutumu rais huyo kwa kutishia vyombo vya sheria kabla ya kufanyika kwa uchaguzi muhimu ili kuongeza muda wa utawala wake baadae mwaka huu.