1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

ISLAMABAD: Watu 10 wauwawa kwenye machafuko

7 Aprili 2007
https://p.dw.com/p/CCBh

Watu 10 wameuwawa na wengine kadhaa kujeruhiwa kufuatia mapigano baina ya wapiganaji wa kisunni na kishia katika mji wa Parachinar kaskazini magharibi mwa Pakistan.

Mapigano yalizuka wakati watu waliokuwa na bunduki walipoanza kuwafyatulia risasi waumini wa madhehebu ya Shia karibu na msikiti mjini Parachinar, mji unaopatikana yapata kilomita 25 kusini magharibi mwa mji wa Peshwar, ambao ni mji mkuu wa jimbo la North West Frontier, linalopakana na Afghanistan.

Maafisa wa serikali katika eneo hilo wametangaza amri ya kutotembea nje na kutaka wanajeshi wapelekwe kusaidia kuyazima machafuko hayo. Wakaazi wanasema hali ya wasiwasi imekuwa ikiongezeka mjini Parachinar katika siku chache zilizopita.