1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Israel yasubiri uongozi mpya

13 Agosti 2008

Lakini bado nafasi ya matumaini katika amani ya Mashariki ya kati ni ndugu.

https://p.dw.com/p/EwRa
Waziri mkuu wa Israel Ehud Olmert (kulia) akiwa na waziri wake wa mambo ya nchi za nje Israeli Prime Minister Ehud Tzipni LivniPicha: AP

Israel inajiandaa kuwa na kiongozi mpya baada ya tangazo la waziri mkuu Ehud Olmert kwamba ataachia madaraka, pale chama chake KADIMA kitakapomchagua kiongozi mpya tarehe 17 mwezi ujao wa Septemba . Lakini tayari wachambuzi wanaashiria kwamba kwa yeyote atakayechukua uongozi, mwenendo wa amani utakabiliwa na changamoto kubwa.

Ukosefu wa matumaini unaelezwa na wengi katika eneo la mashariki ya kati. Mhadhiri wa elimu ya siasa na mratibu wa mpango wa utafiti kuhusu masuala ya Israel katika chuo kikuu cha Cairo Abdelaziz Shadi amesema kwamba sera za Israel hazitobadilika chini ya waziri mkuu mpya. Anaamini kuwa kiongozi yeyote mpya au chama chochote kitaendelea na sera zile zile za kawaida ikiwa ni pamoja na ujenzi wa makaazi mapya kinyume cha sheria.

Itakumbukwa Julai 30 mwaka huu, waziri mkuu Olmert alitangaza kwamba atajiuzulu uwaziri mkuu baada ya uchaguzi katika chama chake KADIMA, kumtafuta kiongozi mpya. Umaarufu wa Olmert umepungua tangu Israel iliposhindwa vibaya kijeshi mbele ya wapiganaji wa Hezbollah nchini Lebanon na kuzidi kuanguka miezi ya karibuni baada ya kuandamwa na mlolongo wa madai ya kuhusika katika visa vya rushwa.

Olmert ambaye alichukua uongozi wa Israel baada ya kuungua mtangulizi wake Ariel Sharon mapema 2006, hakuweza kupiga hatua kubwa sana katika sera ya kigeni na hasa kuhusiana na mwenendo wa amani ya mashariki ya kati.

Hivi sasa Olmert anatarajiwa kubakia kama Waziri mkuu hadi uchaguzi utakapofanyika katika chama chake Septemba 17, Kama atakayerithi wadhifa huo atashindwa kuunda serikali ya mseto, basi Olmert anaweza kubakia madarakani hadi utakapoitishwa uchaguzi wa mapema mwezi Machi 2009. Kwa hivi sasa chama chake cha KADIMA kina viti 29 tu katika bunge la viti 120.

Wagombea wakuu wa uongozi wa chama ni waziri wa mambo ya nchi za nje Tzipni Livni na Waziri wa uchukuzi Shaul Mofaz. Ni Bibi Livni anayetajwa kuwa na nafasi kubwa ya kuibuka mshindi.

Vyama kadhaa vyengine vya kisiasa vinasubiri pembeni kucheza turufu ya uwezekano wa kuunda serikali ya mseto. Usoni kabisa ni kile cha Leba kinachoongozwa na Ehud Barak na Mwenyekiti wa chama cha Likud Benjamin Netanyahu ambaye anapinga maridhiano ya aina yoyote na wapalestina.

Mtaalamu Shadi wa chuo kikuu cha Cairo akiitathimini hali ya kisiasa nchini Israel anasema lakini siku za Netanyahu zimekwisha na anataja kuvunjwa moyo kwa waisraili na uongozi wake miaka ya 1990 alipokua waziri mkuu.

Pia siku za kihistoria katika chama cha Leba za kuwa na viongozi imara kama hayati Izhak rabin pia zimemalizika. Anahoji kuwa kwa sasa vyama vyote havina viongozi imara.Hata hivyo kwa yeyote atakayeshika hatamu kuiongoza serikali ijayo nchini Israel, hakuna matarajio makubwa miongoni mwa wachambuzi ya kuweko mabadiliko yoyote katika sera ya Israel kuelekea wapalestina. Kwa hivyo bado changamoto ni kubwa katika suala la amani ya mashariki ya kati.