1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Baraza la Seneti la Italia kuamua tarehe ya hatma ya Conte

Angela Mdungu
13 Agosti 2019

Baraza la Seneti la Italia, litapiga kura leo, kuamua kuhusu tarehe ya kupiga kura ya kutokuwa na imani na waziri mkuu Giuseppe Conte

https://p.dw.com/p/3Np4I
Giuseppe Conte
Picha: picture-alliance/dpa/ZUMAPRESS/V. Livieri

Baraza la Seneti la Italia, linatarajiwa kupiga kura leo, kutoa maamuzi kuhusu tarehe ya kupiga kura ya kutokuwa na imani na waziri mkuu wa nchi hiyo Giuseppe Conte. Hatua hiyo ni baada ya mkutano wa jana Jumatatu kushindwa kuamua juu ya tarehe hiyo ya kupiga kura ya kutokuwa na imani na waziri mkuu Conte.

Wengi wa wajumbe wa bunge la seneti, walipendelea tarehe ya kupiga kura ya kutokuwa na imani na waziri mkuu wa Italia Giuseppe Conte kuwa Agosti 20. Hivi sasa, bunge hilo linarejea kazini baada ya mapumziko ya majira ya joto na linatakiwa kupiga kura hiyo katika kipindi cha bunge kitakachoanza saa kumi na mbili jioni.

Hatua ya kura hiyo ilichochewa na msaidizi wa waziri mkuu ambaye pia ni waziri wa mambo ya ndani, Matteo Salvini wa chama cha mrengo wa kulia ambaye anasema tofauti za chama chake na chama cha Five star Movement (M5S), Vuguvugu la Nyota tano, ambavyo vinaunda serikali ya umoja zimekuwa kubwa mno na kwamba uchaguzi wa haraka ndiyo njia pekee ya kusonga mbele. Akizungumzia tofauti hizo, Salvini amesema

anataka neno ndiyo liwe kipaumbele katika maeneo kadhaa yakiwemo miradi mikubwa ya miundombinu, makato ya kodi, mabadiliko katika suala la kodi, mabadiliko kwenye mahakama, elimu, maadili, na masuala ya familia yapewe kipaumbele. Salvini ameongeza kuwa, katika miezi ya hivi karibuni, washindwa kufanya mengi kwasababu ya misimamo tofauti.

Matteo Salvini
Waziri wa mambo ya ndani wa Italia, Matteo SalviniPicha: Getty Images/AFP/A. Solaro

Chama cha M5S kimeshiriki kwenye uongozi kwa chini ya mwaka mmoja na kilijikuta katika hali ya sintofahamu wiki iliyopita baada ya wanachma wake kupiga kura wakipingana bungeni juu ya muswada kuhusu mradi ghali.

Nini kitafuata iwapo waziri mkuu Conte ataondolewa na kura ya kutokuwa na imani naye?

Iwapo waziri mkuu Conte atashindwa baada ya kura ya kutokuwa na imani naye kupigwa na serikali kuanguka,itakuwa ni juu ya Rais Sergio Matarella ambaye anatakiwa kuamua, kuhusu uwezekano wa kuitisha uchaguzi mpya  ama kumualika kiongozi wa chama kingine ili wajaribu kuunda serikali.

Chama cha Salvini ni maarufu kwa msimamo wake dhidi ya wahamiaji. Vyama vyenye mrengo kama wa chama chake, viliongoza katika uchaguzi wa Umoja wa ulaya wa mwezi Mei. Hii itamwezesha kuunda serikali ya pamoja na vyama vya mrengo wa kulia.