1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jeshi latoa saa 48 Misri

Admin.WagnerD1 Julai 2013

Hali inazidi kutokota nchini Misri huku jeshi la nchi hiyo likitoa muda wa masaa 48 kwa wanasiasa kutafuta suluhu ya mgogoro unaoendelea nchini humo vinginevyo liingilie kati.

https://p.dw.com/p/18zro
Opponents of Egypt's Islamist President Mohammed Morsi protest outside the presidential palace, in Cairo, Egypt, Sunday, June 30, 2013. Hundreds of thousands of opponents of Egypt's Islamist president poured out onto the streets in Cairo and across much of the nation Sunday, launching an all-out push to force Mohammed Morsi from office on the one-year anniversary of his inauguration. Fears of violence were high, with Morsi's Islamist supporters vowing to defend him. (AP Photo/Hassan Ammar)
Ägypten Proteste in Kairo 30. JuniPicha: picture-alliance/AP

Katika taarifa yake iliyotangazwa kupitia televisheni, mkuu wa jeshi hilo Jenerali Abdel-Fatah el-Sisi amezitaka pande zote kusikiliza matakwa ya raia na kuongeza kuwa matakwa hayo yasipotekelezwa ndani ya masaa 48 yaliyotolewa, basi jeshi litalaazimika kutafuta suluhu yake lenyewe. Es-Sisi pia ameyaita maandamano ya siku ya Jumapili kuwa kielelezo kisio kifani cha matakwa ya umma.

Mkuu wa majeshi Jenerali Abdel Fattah al-Sisi na rais Mursi.
Mkuu wa majeshi Jenerali Abdel Fattah al-Sisi na rais Mursi.Picha: picture-alliance/dpa

Tamarod nayo yatoa muda wa mwisho

Vuguvugu linaloratibu kampeni ya kumuangusha rais Mursi la Tamarod lilisema katika taarifa iliyowekwa kwenye tovuti yake kuwa linampa rais huyo hadi Jumannne saa 11 jioni awe ameondoka madarakani na kuruhusu taasisi za kitaifa kuandaa uchaguzi wa mapema wa rais. Vinginevyo, liliongeza vuguvugu kuwa muda huo ndio utakuwa mwanzo wa kampeni ya uasi wa umma.

Afisa wa ngazi ya juu serikalini amesema kuwa mawaziri wanne -- wa Utalii, Mazingira, mawasiliano na masuala ya kisheria-- wamekabidhi barua zao za kujiuzulu kwa waziri mkuu Hisham Qandil. Hata hivyo, mawaziri wote waliojizulu si kutoka vyama vinavyomuunga mkono rais Mursi, lakini kujiuzulu kwao ni pigo kwa rais huyo, ambae tangu aingie madrakani amekuwa akipambana na idara ya mahakama, vyombo vya habari na polisi, ambavyo anavishtumu kwa kuhujumu juhudi za serikali yake.

Mabango yanayohamasisha uasi dhidi ya rais Mursi.
Mabango yanayohamasisha uasi dhidi ya rais Mursi.Picha: Reuters

Ofisi za udugu wa Kiislamu zachomwa moto na kuporwa

Baada ya maandamano ya Jumapili ambayo yalihudhuriwa na pande mbili za wafuasi na wapinzani wa Mursi, kulikuwepo na utulivu kiasi katika maeneo mengi ya nchi hiyo, lakini kuvamiwa kwa makao makuu ya chama cha Udugu wa Kiislamu na waandamanaji waliochoma ofisi hizo moto na kufanya uporaji, kumeonyesha kuongezeka kwa mgawanyiko nchini humo, na kukilaazimisha chama hicho kuzungumzia kuchukua hatua za kujilinda.

Watu wanane waliuawa katika mapigano ya usiku karibu na ofisi za chama cha Udugu wa Kiislamu, ambako walinzi waliwafyatulia risasi vijana waliokuwa wanarusha mabomu ya petroli na mawe, na afisa wa chama hicho alisema maafisa wake waili walijeruhiwa.

Mambo bado

Makundi hasimu yalishikilia misimamo yake baada ya kuonyeshana nguvu siku ya Jumapili katika uwanja wa Tahrir na katika maeneo mengine ya nchi. Waliberali walioandaa maandamano hayo walitangaza kuwa Mursi amepinduliwa na nguvu ya umma, lakini wakampa muda wa mwisho kuondoka ambao ni kesho Jumanne. Mursi ambaye hakuonekana mwenyewe, alirejea wito wa majadiliano na kuahidi kufanya kazi na bunge jipya litakalochaguliwa ikiwa mgogoro kuhusu sheria za uchaguzi utatatuliwa.

Makao makuu ya chama cha Udugu wa kiislamu yaliyoharibiwa na kuporwa na waandamanaji.
Makao makuu ya chama cha Udugu wa kiislamu yaliyoharibiwa na kuporwa na waandamanaji.Picha: Khaled Desouki/AFP/Getty images

Lakini upinzani hauna imani na chama cha udugu wa Kiislamu, ambacho wanakituhumu kwa kutumia ushindi wake kadhaa katika chaguzi mbalimbali kujilimbikizia madaraka, na sasa wanataka kuwepo na muundo mpya kabisaa wa sheria za demokrasia ambazo wanasema zimepindishwa katika kipindi cha miaka miwili iliyopita. Ofisi ya rais Mursi imesema itatoa taarifa majira ya saa tatu jioni.

Mwandishi: Iddi Ismail Ssessanga/rtre,afpe
Mhariri: Saum Yusuf