1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

John Kerry atoa asilimia 5 ya mshahara wake kwa msaada

AthmanD5 Aprili 2013

Waziri wa mambo ya nje wa Marekani John Kerry, atakuwa akitoa mchango wa asilimia tano ya mshahara wake kila mwaka, ili kuwanufaisha wafanyikazi wa idara ya serikali ya Marekani.

https://p.dw.com/p/18AQm
Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Marekani John Kerry
Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Marekani John KerryPicha: Reuters

Kerry sasa amejiunga pamoja na Rais wa Marekani, Barack Obama, na viongozi wengine wa Marekani kuonesha mshikamano na wafanyikazi wa serikali hiyo waliolazimika kuchukua likizo isiyokuwa na malipo kama hatua ya kupunguza matumizi.

Siku ya Alhamisi msemaji katika idara ya serikali, Victoria Nuland, aliwaambia waandishi wa habari kwamba Kerry atatoa mchango wa dola 9,175 katika mshahara wake wa dola 183,500 ili kuwanufaisha wafanyikazi wa idara ya serikali ya Marekani.

Rais wa Marekani Barrack Obama
Rais wa Marekani Barrack ObamaPicha: Jack Guez/AFP/Getty Images

Nuland aidha amesema kuna uwezekano fedha hizo zikaenda katika misaada ya wanadiplomasia wa Marekani ambao walijeruhiwa au kuuwawa wakiwa kazini, au zikaenda katika misaada ya watoto wa wafanyikazi.

“Tunaangalia mahali bora na pia pengine fedha zote ziweze kupelekwa mahali pamoja au zigawanywe sehemu mbali mbali za kutoa misaada,” alisema Nuland.

Matumizi ya mashirika ya ulinzi na yale yasiyokuwa ya ulinzi yameshuka katika bodi nzima kufuatia kupungua kwa mchakato unaojulikana kama hatua ya kusafisha. Ili kudumisha kazi za dharura na zenye umuhimu, mashirika mengi yanawalazimisha wafanyikazi wake kuchukua likizo zisizokuwa na malipo.

Siku ya Jumatano, serikali ya Marekani ilisema mchango wa Obama wa asilimia tano aliyojitolea kutoa kutoka kwa mshahara wake wa dola 400,000 ulianza kuchukuliwa kutoka Machi mosi, na itaendelea hadi mwezi Desemba.

Naye msemaji wa waziri wa ulinzi wa Marekani, Chuck Hagel, amesema Hagel atakuwa akitoa msaada wake wa siku 14 za kufanya kazi kwa serikali hiyo, ambayo ni msaada wa takriban dola 10,750.

Waziri wa Ulinzi wa Marekani Chuck Hagel
Waziri wa Ulinzi wa Marekani Chuck HagelPicha: Reuters

Kabla ya kuchukua wadhifa wake wa waziri wa mambo ya nje wa Marekani mapema mwaka huu, Kerry aliorodheshwa kama seneta tajiri sana nchini Marekani, akiwa na kiwango cha pesa kinachokisiwa kuwa kati ya dola milioni 184 na dola milioni 288 mwaka 2011.

Kerry mwenye umri wa miaka 69 alirithi pesa zake kutoka kwa familia ya mamake. Kerry amemuoa Teresia Heinz, ambaye ni mjane aliyerithi mali nyingi baada ya mumewe wa kwanza, John Heinz, kufariki.

Mwandishi: Dalila Athman/REUTERS/AFP

Mhariri: Josephat Charo