1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jukumu la kutumukia jeshini lawekewa suala la kuuliza

Oumilkher Hamidou14 Septemba 2010

Wahariri wamemulika jinsi waapiga kura wa vyama vya kihafidhina walivyogawika katika suala la kufutiliwa mbali jukumu la vijana kutumikia jeshini

https://p.dw.com/p/PBfF
Waziri wa ulinzi zu Guttenberg (kulia) na mkuu wa vikosi vya wanajeshi Volker WiekerPicha: AP

Jukumu la kila kijana wa kiume kulitumikia jeshi anapokamilisha umri wa miaka 18 na msichana akiwa atapendelea kufanya hivyo na jinsi ya kujikinga dhidi ya mgogoro kama ule ulioitikisa sekta ya fedha kuanzia mwaka 2008 ni miongoni mwa mada zilizochambuliwa zaidi na wahariri wa magazeti ya Ujerumani hii leo.

Tuanzie lakini jeshini ambako chama cha Christian Democratic Union CDU kimeamua kuunga mkono mageuzi yaliyopendekezwa na waziri wa ulinzi Karl-Theodor zu Guttenberg.Gazeti la mjini Berlin "Berliner Zeitung linaandika:

"Wana Christian Democratic wanahoji ukosefu wa usawa jeshini ndio sababu ya kupitisha uamuzi huo,hoja hizo lakini ni kujitoa kimaso maso tuu ili kutuliza nyoyo za wapiga kura wa kihafidhina wasiojua nini la kufanya.Katika kipindi cha miaka 50 iliyopita,wapiga kura wamekua wakiamini kuwa jukumu la kutumikia jeshini na raia anaevalia sare ya kijeshi ni kitambulisho cha fahari ya kihafidhina.Kitambulishio hicho sasa kinatokeweka kutokana na hatua za kufunga mikaja,kwasababu waziri wa ulinzi Karl-Theodor zu Guttenberg wa kutoka chama cha CSU,amegundua kwamba jeshi la shirikisho halitaweza miaka ijayo kupata bajeti ile ile na kwamba atalazimika kumuomba fedha ziada Wolfgang Schäuble.

Gazeti la "Nürnberger Nachrichten linaandika:

Kansela Angela Merkel pia amenaswa na mtego wa zu Guttenberg.Waziri huyo amemuonyesha mkubwa wake jinsi mtu anavyoweza kugundua na kutekeleza mambo bila ya ugonvi wa miezi kadhaa miongoni mwa washirika serikalini.Hivyo hasa ndivyo wengi miongoni mwa wapiga kura waliovunjia moyo walivyokua wakitarajia .Na hasa wale wa kutoka kambi ya kihafidhina wanaohofia kudhoofika kambi yao.Watasikitika ikiwa watu hawatalazimika tena kutumikia jeshini,hata hivyo zu Guttenberg watamsamehe-kwasababu yeye ndie mwanaasiasa pekee aliyesalia kutoka vyama ndugu na ambaye anaziunganisha kambi za mrengo wa kulia za CDU na CSU.

Mada yetu ya mwisho inahusu sheria mpya za kuepusha pasitokee mgogoro mwengine wa fedha ulimwenguni-maarufu kwa jina la Basel nambari tatu.Gazeti la mjini Stuttgart-Stuttgarter Zeitung linaandika:

Muhimu kwa sasa ni kuona kwamba sheria hizo mpya zinatumika pia katika masoko ya fedha na benki kubwa kubwa za dunia.Wakutiliwa shaka zaidi ni Marekani.Ikiwa maridhiano yaliyofikiwa mjini Basel nchini Uswisi hayatatekelezwa kikamilifu nchini Marekani,basi hali hiyo itawafanya walimwengu wapotelewe na imani mbele ya serikali ya Marekani.Kwasababu mgogoro wa hivi karibuni chanzo chake ni huko huko Marekani.

Nalo gazeti la Neue Tag linaandika:

Tangu zama za Thomas Jefferson,muasisi wa tangazo la uhuru wa Marekani,aliyekuja kuwa rais wa tatu wa muungano wa mataifa ya Amerika,alionya miaka 200 iliyopita:Benki ni taasisi hatari kwa uhuru kuliko hata jeshi.Tangu mgogoro wa fedha ulioitikisa dunia miaka miwili iliyopita,onyo hilo limepata pia waungaji mkono kutoka nchi za Ulaya.Hata hivyo ushawishi wa benki umezidi kuongezeka.Sio tuu humu nchini bali pia katika upande wa pili wa bahari ya Atlantik,mgogoro wa fedha umepelekea taasisi za fedha kuungana na kwa namna hiyo kuzidi kuwa na nguvu.Pindi zikiporomoka,zitauporomosha mfumo mzima wa kiuchumi.

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/Inlandspresse

Mpitiaji:Mohamed Abdulrahman