1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jumuia nne za waislam wa Ujerumani zaungana

Oummilkheir11 Aprili 2007

Wizara ya ndani ya Ujerumani yawapongeza waislam kwa kuunda halmashauri kuu

https://p.dw.com/p/CHGU
Waumini wa dini tofauti msikitini
Waumini wa dini tofauti msikitiniPicha: AP

Jumuia nne za waislam wa Ujerumani wameunda halmashauri ushirikiano wa waislam-KRM ili kurahisisha mdahalo kati ya jamii yao na serikali.Hayo ni kwa mujibu wa kiongozi mmojawapo wa baraza hilo Rafet Öztürk.

Jumuia ya waislam wa Uturuki na taaluma za kidini-DITIB,baraza la dini ya kiislam- Islamrat-baraza kuu la waislam wa Ujerumani Zentralrat der Musalime na jumuia ya vyama vya tamaduni za kiislam,wamekubaliana kuunda halmashauri itakayokua na jukumu la kuwakilisha msimamo wao wa pamoja mbele ya serikali.

“Tutapima na kuona kama tunaweza kupitisha maamuzi kwa pamoja au la” amesema Rafet Öztürk,anaesimamia midahalo pamoja na jamii tofauti za kidini ndani ya jumuia ya waislam wa kituruki na taaluma za kidini DITIB.

Wawakilishi wa jumuia hizo nne wamekubaliana kwamba wakuu wa jumuia hizo wawe wanabadilishana zamu kila baada ya miezi sita wakikabidhiwa wadhifa wa msemaji wa halmshauri hiyo mpya.

Wizara ya ndani ya serikali kuu ya Ujerumani imesifu uamuzi wa kuundwa halmashauri kuu ya ushirikiano wa waislam wa Ujerumani KRM.Msemaji wa wizara hiyo amesema mjini Berlin tunanukuu:”Hii ni hatua ya maana iliyopitishwa wakati muwafak”-wiki tatu kabla ya kuitishwa duru nyengine ya mkutano wa taifa kuhusu dini ya kiislam,May pili ijayo.Tunaona waislam wanafanya kila la kufanya kujitenganisha na wenye kupigia upatu matumizi ya nguvu”.Mwisho wa kumnukuu msemaji wa wizara ya mambo ya ndani ya serikali kuu ya ujerumani mjini Berlin.

Kwa mujibu wa takwimu, kuna zaidi ya waislam milioni tatu na laki mbili wanaoishi nchini Ujerumani-laki tatu kati yao wamejiunga na jumuia za kiislam.Jamii kubwa kabisa ya kiislam ni ya waturuki,wamnaofikia asili mia 75,wakifuatiwa na wakaazi wa Afrika kaskazini au nchi za Maghreb wanaofikia watu laki mbili,wairan waumini laki moja na waislam wa kutoka Yugoslavia ya zamani wanaokadiriwa pia kufikia watu laki moja.

Jumuia kubwa kabisa ya waislam nchini Ujerumani ni ile ya DITIB-ambayo wafuasi wake ni wa madhehebu ya sunni-na iko chini ya usimamizi wa wizara ya Uturuki ya taaluma za kidini-jumuia yenye wanachama laki moja na 30 elfu na mashirika 860 nchini Ujerumani.

Baraza la dini ya kiislam au Islamrat kama linavyoitwa kijerumani ni mchanganyiko wa vyama 37 vya kidini likiwa na wanachama 40 elfu na kuongozwa na shirika la Milli Görüs-kwa mujibu wa idara ya upelelezi ya Ujerumani,katika wakati ambapo baraza kuu la waislam Zentralrat der Muslime lenye mashirika 19 na zaidi ya wanachama 15 elfu,limefanikiwa kujitokeza kama muakilishi anaetangulizwa mbele na serikali kuu ya Ujerumani panapohusika na masuala ya dini ya kiislam.

September 27 iliyopita wawakilishi kama 27 hivi wa mashirika ya serikali na jumuia za waislam walikutana na waziri wa mambo ya andani Wolfgang Schäuble kwa mkutano wa mwanzo wa taifa kuzungumzia masuala yanayohusu dini ya kiislam.

Msemaji wa baraza jipya la ushirikiano wa waislam wa Ujerumani,Ayyub Axel Köhler amesema wanataraji hivi sasa patakua na hali ya usawa kati yao na makanisa na jumuia nyenginezo za kidini.