1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Juu ya uhusiano kati ya Urusi na nchi za Magharibi

Maja Dreyer15 Oktoba 2007

Mkutano kati ya rais Putin wa Urusi na Kansela wa Ujerumani Angela Merkel ni suala muhimu kwenye kurasa za wahariri katika magazeti ya Ujerumani. Basi wanaandika nini?

https://p.dw.com/p/C7lM

Moja kwa moja tuanze na gazeti linalosomwa kwa wingi humu nchini, “Frankfurter Allgemeine”.

“Katika sera za kimataifa, Urusi inataka kuwa na mamlaka katika dunia nzima. Licha ya kwamba namna Rais Putin anavyotawala haiendi sambamba na maadili ya nchi za magharibi, hayo yasiathiri uhusiano kati ya Urusi na Ujerumani. Vilevile kuna maslahi ya pamoja. Bila ya Urusi yenye haki ya kupiga kura ya turufu katika baraza la usalama la Umoja wa Mataifa, mizozo mingi ya kimataifa haitaweza kutatuliwa. Mambo lakini yangekuwa rahisi ikiwa Urusi itakubali kushirikiana badala ya kutaja matakwa yake tu. Kwa hivyo, kuna mengi ya kuzungumzia kwenye mkutano kati ya Kansela Angela Merkel wa Ujerumani na Rais Putin wa Urusi.”

Kabla ya Rais Putin alipowasili Ujerumani, wajumbe wa mashirika mbalimbali ya Ujerumani na Urusi yalikutana kuzungumzia mahusiano kati ya nchi hizo mbili. Mkutano huu chini ya uwenyekiti wa rais wa zamani wa Urusi, Michael Gorbatshov, na waziri mkuu wa mwisho wa Ujerumani Mashirki de Mazière ulizusha masuala mengi. Mhariri wa “Wiesbadener Kurier” anachunguza moja kati yao:

“Suali moja lililozuka kwenye mazungumzo haya ni muhimu sana: Je, Urusi inashukiwa mno na nchi za Magharibi kama Ujerumani? Bila shaka, ni jambo lisilowezekana kuamini kwamba katika nchi iliyotawaliwa na madikteta na wafalme kwa karne kadhaa itaweza kutekeleza sheria za demokrasia katika muda mfupi. Tukumbuke pia kwamba mabadiliko kuelekea demokrasia chini ya Gorbatshov na Yeltzin yalileta michafuko ya kisiasa na kijamii nchini Urusi.”

Na hatimaye juu ya suala hili tusikie maoni ya mhariri wa “Süddeutsche Zeitung”. Huyu anaangalia nyuma kwanza akiandika:

“Katika urafiki kati ya Kansela wa zamani wa Ujerumani Gerhard Schröder na Rais Putin wa Urusi, pande zote mbili zilikuwa na njozi juu ya upande mwingine. Urusi iliamini kwamba Ujerumani itaendesha uhusiano maalum naye bila ya kujali sera za Umoja wa Ulaya. Upande wa Ujerumani kulikuwa na dhana kwamba Urusi iko njiani kuimarisha demokrasia. Lakini kwa sasa hali halisi ni wazi. Ujerumani inauunga mkono msimamo wa Umoja wa Ulaya. Na Urusi inafuata sera za kuonyesha nguvu zake chini ya rais Putin. Kwa hivyo, inambidi Kansela Merkel kutaja kabisa wapi na wapi hakuna maelewano. Urusi na nchi za Magharibi zilirudi katika hali ya kutokubaliana. Ikiwa ni juu ya Iran, Kosovo au mitambo ya kufyetua makombora – kilichokubaliwa ni kwamba hakuna makubaliano.”