1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Keryy awataka Ghani, Abdullah kupatana

11 Julai 2014

Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, John Kerry, amekutana na mahasimu wakubwa kwenye uchaguzi wa rais wa Afghanistan kuwataka wautatue mzozo uliompa ushindi mgombea anayeungwa mkono na rais anayemaliza muda wake.

https://p.dw.com/p/1CbK8
Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, John Kerry (kulia) na kiongozi wa upinzani wa Afghanistan, Abdullah Abdullah.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, John Kerry (kulia) na kiongozi wa upinzani wa Afghanistan, Abdullah Abdullah.Picha: Reuters

Kerry ametumia siku nzima ya leo kukutana na pande zote mbili zinazodai ushindi kwenye uchaguzi wa duru ya pili uliofanyika tarehe 14 Juni na matokeo yake ya awali kutangazwa Jumatatu iliyopita yakimpa ushindi Ashraf Ghani, ambaye wengi wanamchukulia kuwa mtu wa Rais Hamid Karzai.

Hata hivyo, kabla ya kuwasili mjini Kabul hivi leo, Kerry aliweka wazi kwamba matokeo hayo ya kura ndiyo yatakayoamua muelekeo wa Marekani kwa Afghanistan. Akizungumza baada ya mazungumzo yake na Ghani, Kerry alisema kwamba Marekani inataka kuona muafaka ukifikiwa juu ya uhalali wa matokeo hayo.

"Ni muhimu kwamba yeyote anayekuwa rais, awe anatambuliwa na watu kuwa amekuwa rais halali kupitia mchakato wa kidemokrasia na serikali yake iwe ni ile ambayo inaweza kuwaunganisha watu na kuwaongoza kwenye mustakabali wao. Matokeo yaliyotangazwa Jumatatu ni ya awali, hayakuidhinishwa na wala si ya mwisho na hakuna anayestahiki kujitangazia ushindi kwenye hatua hii."

Ghani ataka uhakiki huru pia

Ghani kwa upande wake amemuhakikishia Kerry kwamba upande wake hauna tatizo na kuhakikiwa upya kwa matokeo hayo, madai yanayotolewa na mpinzani wake Abdullah Abdullah, ambaye anaamini yeye ndiye mshindi halali wa uchaguzi huo.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, John Kerry (kushoto) na mgombea aliyetangazwa mshindi, Ashraf Ghani.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, John Kerry (kushoto) na mgombea aliyetangazwa mshindi, Ashraf Ghani.Picha: Reuters

"Dhamira yetu ni kuhakikisha kuwa zoezi la uchaguzi linapata uhalali na heshima kutoka kwa watu wa Afghanistan na dunia. Kwa hivyo tunaamini kwamba panapaswa kuwepo na uhakiki wa kina na wa ndani kurejesha imani," Ghani alimwambia Kerry.

Marekani huipa nchi hiyo iliyoivamia kijeshi zaidi ya miaka 10 iliyopita, msaada mkubwa wa kifedha na kijeshi katika jitihada za kuijenga upya na kuimarisha taasisi zake za kiserikali na kijamii.

Lakini kukataa kwa Abdullah kuyatambua matokeo hayo, kunachukuliwa kama hatua inayoweza kurejesha mapambano makubwa ya kikabila na kiitikadi, katika nchi ambayo hadi sasa haijaweza kuudhibiti uasi wa kundi la wanamgambo la Taliban.

Abdullah asisitiza uhakiki kufanyika

Naye, Abdullah, mara tu baada ya kukutana na Kerry alirejelea tena msimamo wake wa kuona kura ya wananchi wa Afghanistan ikiheshimiwa.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, John Kerry (kulia) na Rais Hamid Karzai wa Afghanistan.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, John Kerry (kulia) na Rais Hamid Karzai wa Afghanistan.Picha: Reuters

"Mustakabali wa mafanikio yetu unategemea kufanikiwa kwa mchakato wa kidemokrasia. Sio idadi ya wanajeshi na wala si chengine chochote. Miaka 13 iliyopita, hali ilikuwa tafauti kwenye nchi hii, lakini kisha tukawa na ukabidhianaji wa madaraka kwa njia za amani kwa sababu tulikusudia kuingia kwenye mchakato wa kidemokrasia," alisema Abdullah.

Bado haijatangazwa rasmi lini uhakiki huo wa matokeo ya kura yaliyompa Ghani ushindi wa zaidi ya kura milioni moja mbele ya Abdullah utakapofanyika.

Marekani inataka matokeo rasmi yasitangazwe kabla ya kwanza kuhakikiwa na chombo huru, kama vile Umoja wa Mataifa.

Mwandishi: Mohammed Khelef/Reuters/AFP
Mhariri: Saumu Yusuf